Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 12:59

IEBC yasema mifumo yake iko salama


Maafisa wa IEBC wakithibitisha kura katika makao makuu Bomas, mjini Nairobi, Kenya.
Maafisa wa IEBC wakithibitisha kura katika makao makuu Bomas, mjini Nairobi, Kenya.

Tume ya uchaguzi na mipaka nchini Kenya, IEBC, Jumanne iliwahakikishia wapiga kura kwamba vifaa na mifumo ya kupigia kura, iko imara.

Hali ya wasiwasi ilitanda katika baadhi ya maeneo punde tu baada ya habari kuenea kwamba naibu Mkurugenzi wa kitengo cha mawasiliano na teknolojia, Chris Msando wa tume ya IEBC, aliuawa katika kitongoji cha jiji la Nairobi, katika mazingira ya utatanishi.

Licha ya Inspekta Mkuu wa Polisi Joseph Boinnet kuwatahadharisha Wakenya dhidi ya kueneza uvumi kuhusina na kifo hicho, baadhi ya viongozi wa kisiasa waliendelea kushinikiza serikali kufanya uchunguzi wa kina. Wengine wamedai kwamba huenda afisa huyo alikuwa na habari muhimu kuhusu mfumo wa teknolojia unaotumiwa na tume hiyo kuelekea uchaguzi wa mwaka huu.

Mmoja wa vinara wa muungano wa NASA, Musalia Mudavadi, amewaambia waandishi wa habari nje ya ofisi za Muungano huo katika eneo la Upper Hill, jijini Naironi kuwa: "Ni wazi kwamba mtu huyo muhimu mno, ambaye labda alikuwa na password muhimu mno, ameuawa wakati huu muhimu wa uchaguzi.

Alikuwa anasimamia kitengo muhimu mno kilicho na rekodi zote za kidijitali, na alitarajiwa kuongoza zoezi la kuhakikisha kwamba mfumo huo wa kielektroniki ulikuwa shwari na tayari kwa uchaguzi wa wiki ijayo."

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Tume ya IEBC, Wafula Chebukati, amewahakikishia Wakenya kwamba mifumo na vifaa vyote vya IEBC vIko imara na tayari kwa uchaguzi.

"Mifumo yetu iko salama," alisema Chebukati na kuongeza: "Tunawatoa huduma wetu na hapo siku ya uchaguzi, tutatoa matokeo kama tunavyotarajiwa kufanya."

Siku ya Jumanne, Rais Uhuru Kenyatta pia alijiunga na wengine kutoa kauli ya kulaani mauji hayo,na kuamuru kwamba maafisa waandamizi wa IEBC wapewe ulinzi wa ziada.

Lakini Muungano wa NASA uliitaka jumuiya ya kimataifa kuingilia kati na kusaidia katika uchunguzi wa kifo cha afisa huyo wa IEBC.

Haya yalijiri katika siku ambayo kampuni ya Infotrack ilitoa uchunguzi wake wa mwisho wa maoni kuhusu uchaguzi wa urais, na kueleza kwamba mgombea wa muungano wa NASA, Raila Odinga, alikuwa anaongoza kwa asilimia 48 ya wale waliohojiwa, huku rais Uhuru Kenyatta akimfuata kwa karibu, akiwa na asili mia 47 ya kura.

Jumanne ndiyo siku ya mwisho kwa mashirika ya kutoa kura za maoni, kutoa matokeo yao.

XS
SM
MD
LG