Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 01:56

IEBC: Tuliharakisha kutangaza matokeo ya uchaguzi wa urais kwa sababu usalama wetu ulikuwa hatarini


Mwenyekiti wa tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC Wafula Chebukati akitangaza matokeo ya kura za urais Aug 15 2022. Picha: AP
Mwenyekiti wa tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC Wafula Chebukati akitangaza matokeo ya kura za urais Aug 15 2022. Picha: AP

Tume huru ya uchaguzi na mipaka ya Kenya IEBC imesema kwamba ililazimika kutangaza matokeo ya uchaguzi wa urais kwa ‘haraka’ kwa sababu mazingira na usalama wa wafanyakazi wake vilikuwa katika hali ya hatari.

Wakili wa IEBC George Murugu, ameiambia mahakama kwamba uamuzi wa kutotangaza matokeo ya kura katika maeneo bunge 27 ulifikiwa kwa sababu makamishna wa IEBC walikuwa wanakabiliwa na vitisho vya ukosefu wa usalama, na hivyo hesabu ya kura hizo ilijumulishwa bila kutangazwa lakini yalikuwa yamefanyiwa uhakiki.

Murugu ameieleza mahakama kwamba matokeo hayo yalikuwa tayari kutangazwa na kamishna Prof Abdi Guliye, lakini vurugu zilitokea katika ukumbi wa Bomas, na hivyo uamuzi ukafikiwa kwamba ilikuwa jambo la busara kutangaza matokeo ya jumla ya kura za urais.

“Mwenyekiti wa IEBC alifanya uamuzi huo kutokana na hatari ya usalama iliyokuwa inaonekana, maafisa wa uchaguzi wakiwa wametishiwa kukamatwa, wengine tayari walikuwa wametekwa nyara na kujeruhiwa,”

Wakili Murugu anamuwakilisha mwenyekiti wa tume ya uchaguzi Wafula Chabukati.

Mbona matokeo yalitangazwa siku moja kabla ya siku ya mwisho ya kufanya hivyo

Kuhusu swali aliloulizwa na jopo la majaji 7 kilichopelekea matokeo ya urais kutangazwa siku moja kabla ya siku ya mwisho iliyowekwa kikatiba, wakili Murugu amesema kwamba kazi ya kuhesabu na kuhakiki matokeo ya uchaguzi ni ya tume hiyo, na kwamba kazi hiyo ilikuwa inaendeshwa vizuri ikiwemo kutangazwa kwa wakenya kwamba matokeo yangetangazwa siku hiyo.

Amemtetea mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati kutokana na shutuma kwamba alikuwa anaendesha tume hiyo kwa njia ya kibabe, akisistiza kwamba makamishna wote walishiriki katika mchakato mzima wa uchaguzi, kuhesabu, kuhakiki na kutangaza matokeo.

Amesema kwamba makamishna 4 wanaodai kwamba walikuwa wamepewa majukumu yasiyoeleweka, walionekana na wakenya wote wakisoma matokeo ya uchaguzi wa urais mara kwa mara.

XS
SM
MD
LG