Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 10:00

Hali ya Bobi Wine yaendelea kuwa mbaya


Bobi Wine (Wapili kushoto) akiwa mahakama ya mwanzo Gulu, Kaskazini mwa Uganda, Agosti 23, 2018.
Bobi Wine (Wapili kushoto) akiwa mahakama ya mwanzo Gulu, Kaskazini mwa Uganda, Agosti 23, 2018.

Hali ya mwanamuziki mashuhuri Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine imeendelea kuwa mbaya ambapo hivi sasa anashindwa kusimama kutokana na kupigwa na vyombo vya usalama nchini Uganda.

Akiwa kati ya waliopewa dhamana Jumatatu, Bobi Wine amefunguliwa mashtaka ya uhaini kufuatia madai kwamba yeye na wanasiasa wenzake kuhusishwa na kuutupia mawe msafara wa Rais Yoweri Museveni mwezi Agosti.

Jaji wa Mahakama Kuu Uganda amewapa dhamana Jumatatu wanasiasa hao 12 wa chama cha upinzani.

Kyagulanyi, ambaye alichaguliwa kuwa mbunge 2017, hivi sasa anashindwa kusimama baada ya kupigwa wakati akiwa kizuizini, wakili wake ameliambia shirika la habari la Reuters wiki iliyopita, akitoa maelezo ya ndugu zake waliomtembelea.

Serikali ya Uganda inasema kuwa tuhuma za kupigwa kwake ni “upuuzi mtupu.”

Kuwekwa kizuizini kwa Kyagulanyi na wanasiasa wengine ambao wamekuwa wakimkosoa Museveni kuliibua siku mbili za maandamano katika mji mkuu Kampala na maeneo mengine nchini Uganda wiki iliyopita.

Watuhumiwa hao 12 walikanusha mashtaka dhidi yao. Dazeni ya watu wengine pia wamefunguliwa mashtaka ya uhaini kuhusiana na madai ya kuhusika na kuutupia mawe msafara huo.

“Watuhumiwa wote 12 wamepewa dhamana. Nitaweka masharti zaidi juu ya dhamana yao baadae,” Jaji wa Mahakama Kuu Stephen Mubiru amesema katika kesi iliyorushwa na televisheni mubashara.

Kila aliyeomba dhamana ametakiwa kulipa Shilingi milioni 5 za Uganda ($1,340), zitakazo chukuliwa iwapo watashindwa kuja mahakamani tena. Mwendesha mashtaka wa serikali hakupinga watuhumiwa hao kupewa dhamana.

Kyagulanyi, mwanamuziki mashuhuri, ametunga nyimbo kadhaa ambazo zimekuwa zikikosoa serikali ya Museveni na kumpatia msanii huyo wafuasi wengi.

Jaji Mubiru aliamuru watuhumiwa hao 12 kupelekwa katika mahakama ya chini Agosti 30, lakini pia alikataa ombi kutoka kwa mwendesha mashtaka kwamba pasipoti zao zizuiliwe.

Wakati kesi inasikilizwa mahakamani, Shaban Atiku, mmoja wa watuhumiwa alizimia.

Kizza Besigye, kiongozi wa upinzani, ambaye alikuwa mahakamani alijiunga katika kutoa huduma ya kwanza kumsaidia mtuhumiwa aliyezimia mahakamani.

XS
SM
MD
LG