Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 26, 2024 Local time: 14:55

Gambia yarejea kwa masharti ya kusalia nyumbani usiku baada ya maambukizi ya Corona kuongezeka


Makamu wa Rais wa Gambia Isatou Touray aliyeambukizwa virusi vya Corona mwezi Julai.
Makamu wa Rais wa Gambia Isatou Touray aliyeambukizwa virusi vya Corona mwezi Julai.

Gambia, nchi ndogo zaidi barani Afrika, imetangaza tena masharti ya watu kusalia nyumbani wakati wa usiku kwa mda wa wiki tatu.

Hii ni baada ya kiwango cha maambukizi ya virusi vya Corona kuongezeka kwa asilimia 60 katika mda wa wiki moja na kufikia watu 800.

Maafisa wa afya wanasema ongezeko la maambukizi ya virusi vya corona linatokana na hali ya watu kutozingatia maagizo ya kujizuia na maambukizi.

Maafisa wameimarisha shughuli za upimaji kujua watu walioambukizwa virusi hivyo hatari.

Jumla ya watu 16 wamekufa nchini Gambia kutokana na maambukizi ya virusi vya Corona.

Amri ya watu kutotoka nyumbani kwao inaanza kutekelezwa kuanzia saa nne usiku hadi saa kumi na moja asubuhi kuanzia Leo alhamisi.

Mikusanyiko ya watu pia imepigwa amarufuku.

Msemaji wa serikali Ebrima Sankareh amesema kwamba masoko yametakiwa kufunga shughuli ifikapo saa nane mchana.

Polisi watashika doria kuhakikisha kwamba masharti hayo yanatimizwa.

Maafisa wametakiwa kushika doria kwenye mpaka wa Gambia na Senegal na wageni wote wanaoingia Gambia kupimwa ili kutambua iwapo wameambukizwa virusi hivyo.

Zaidi ya watu 10,500 wameambukizwa virusi vya Corona nchini Senegal.

Waziri wa maswala ya Wanawake, Jamii na Watoto Fatou Kinteh, ameambukizwa virusi vya Corona na kuwa waziri wa nne kuambukizwa virusi hivyo nchini Gambia katika mda wa wiki moja.

Makamu wa rais Isatou Touray, aligunduliwa kuambukizwa virusi hivyo Julai 29 na kulazimu rais Adama Barrow kuwekwa karantini.

Serikali imesema kwamba rais Barrow hajaambukizwa.

Wizara ya afya imesema kwamba watu sita waliothibitishwa kuambukizwa virusi vya Corona hawajulikani walipo baada ya kutoroka kutoka kwa kituo cha matibabu katika mji mkuu.

Imetayarishwa na Kennes Bwire, VOA, Washington DC

XS
SM
MD
LG