Mkuu wa sera za mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell amesema anatumai kutakuwa na makubaliano wiki hii kwa Russia kuzifungulia bandari za Ukraine huko Odesa na kwingineko, huku maisha ya maelfu ya watu yakitegemea makubaliano hayo huku kukiwa na uhaba wa chakula katika nchi nyingi.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Brussels, Borrell alisema Russia inapaswa kuruhusu mauzo ya nafaka ya Ukraine la sivyo jumuiya ya kimataifa italazimika kusema Russia inatumia chakula kama silaha bila kuzingatia maisha ya binadamu.
Sio mchezo wa kidiplomasia. Ni suala la maisha na kifo kwa wanadamu wengi, Borrell alisema.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema wiki iliyopita kuna makubaliano mapana juu ya mpango kati ya Russia na Ukraine, na Uturuki na Umoja wa Mataifa, wa kuuza nje mamilioni ya tani za nafaka za Ukraine zilizokwama kwenye maghala tangu uvamizi wa Russia Februari 24.