Makundi ya upinzani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yameitisha mgomo wa kitaifa Jumanne, kwa matumaini kwamba watamlazimisha rais Joseph Kabila wa nchi hiyo, kujiuzulu baada ya muhula wake wa pili kumalizika mnamo mwishoni mwa mwaka huu.
Haya yamejiri baada ya upinzani kususia mazungumzo yaliyoitishwa na Umoja wa Afrika mwishoni mwa wiki, na ambayo yangekuwa chini ya uenyekiti wa waziri mkuu wa Togo, Edem Kodjo.
Martin Fayulu, ambaye ni kiongozi wa chama cha Commitment for Citizenship and Development na mwanachama wa muungano wa upinzani, alidai kuwa Kodjo anampendelea rais Kabila na hivyo basi hawezi kusimamia mazungumzo hayo.
Fayulu alisema kuwa upinzani unaweza tu kushiriki katika mazungumzo chini ya azimio la baraza la Usalama la umoja wa mataifa, ambalo, alisema, lilitaka mazungumzo yanayoheshimu katiba ya Kongo.