Ingawa Cameroon imepongezwa kwa hatua zake za kijeshi katika kukabiliana na kundi la Boko Haram na kulisukuma nje kutoka kwenye eneo la kasakazini na katika nchi jirani ya Nigeria, shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limekosoa vikosi vya usalama vya Cameroon kutokana na uhalifu ikiwa pamoja na mauaji holela, mateso na pia kuwashikilia wafungwa katika mazingira yasiyo ya kibinadamu.
Kwenye ripoti iliopewa kichwa cha habari ‘Right Cause, Wrong Means’ iliyochapishwa wiki iliopita, shirika la Amnesty limesema kuwa zaidi ya watu 1,000 wanaoshukiwa kuliunga mkono Boko Haram wamezuiliwa kwenye mazingira mabaya, wengi wakiwa kwenye jela ya Maroua ilioko kaskazini mwa Cameroon.
Jela hiyo ilijengwa kuhudumia wafungwa 350 lakini sasa hivi ina zaidi ya wafungwa 1,500. Amnesty inasema kuwa hadi watu 8 hufa kila mwezi katika jela hiyo kutokana na mazingira duni.