Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 09:12

Biden apinga madai ya Trump juu ya kupatikana chanjo karibuni


Rais wa Marekani Donald Trump (kulia) na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.
Rais wa Marekani Donald Trump (kulia) na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.

Mgombea wa urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democratic, Joe Biden alifanya mkutano wake wa kwanza ulioandaliwa na CNN Alhamisi na kupinga waziwazi pendekezo la rais Donald Trump kwamba chanjo ya virusi vya corona huenda itapatikana wiki chache tu zijazo.

Biden amewaonya Wamarekani kuwa wasimuamini Rais Trump. Naye Rais Trump alikuwa katika jimbo muhimu la Wisconsin ambako alitangaza duru mpya ya msaada kwa wakulima wa kiasi cha dola bilioni 13 kwa sababu ya janga.

Biden na Trump wote watasafiri kwenda Minessota Ijumaa siku ya kwanza ya upigaji kura wa mapema katika jimbo hilo.

Mkutano huo ambao ulionyeshwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha CNN ni wa kwanza ambao Biden ameufanya tangu akubali uteuzi wa chama cha Democratic kuwania urais mwezi uliopita, na kuwapa watazamaji fursa ya nadra kumuona akijibu maswali kutoka kwa watu ambao ana matumaini watampigia kura mwezi Novemba.

Joe Biden akijibu maswali kutoka kwa washiriki wa mkutano ulioandaliwa na Kituo cha Televisheni CNN ulioongozwa na mtangazaji wa kituo hicho Anderson Cooper
Joe Biden akijibu maswali kutoka kwa washiriki wa mkutano ulioandaliwa na Kituo cha Televisheni CNN ulioongozwa na mtangazaji wa kituo hicho Anderson Cooper

CNN ilipanga mkutano huo nje ya uwanja wa mpira wa baseball ambapo washiriki waliegesha magari yao na kubaki kando yake wakiuliza maswali, ili kuhakikisha usalama wao wa kutokaribiana.

Biden alitumia muda mwingi jana usiku kumshambulia Trump jinsi alivyoshughulikia janga hili, ikiwa ni pamoja na rais kukiri mwenyewe kwa mwandishi wa habari Bob Woodward kwamba alipuuza umuhimu ya ugonjwa huu unaosababisha vifo.

Mgombea urais kwa tiketi ya chama cha Demokratik Biden alieleza : "Hakutaka kuona jambo lolote linatendeka. Yeye (rais) anataka tu achaguliwe tena. inabidi iwe kuhusu maslahi ya wamarekani kwani wako katika matatizo. Kama hatufanyi hivyo tutakuwa matatani."

Aliongeza kusema : "Na kwa upande mwngine,hivi karibuni alitoa matamshi tofauti na mkurugenzi wake mwenyewe wa CDC. Amesema, kwa hakika, ukivaa barakoa pekee yake, hakuna chochote kingine isipokuwa hii barakoa, basi utaokoa maisha kati ya sasa na Januari, maisha ya watu laki moja, na ni vyema tuwe wakweli na watu wa Marekani.”

Trump akizungumza huko Mosinee, mji uliyopo katikati mwa jimbo la Wisconsin, ambako maafisa wa jimbo wameripoti watu wengine 2,000 waliambukizwa na virusi vya corona, siku ya Alhamisi ikiwa ni ongezeko kubwa kwa siku moja.

Katika Uchaguzi uliopita Trump alimshinda Mdemokrat Hillary Clinton huko Wisconsin 2016 kwa chini ya asilimia moja ya kura, na kubainisha kwa mara ya kwanza kuwa jimbo hili lilimpigia kura Mrepublican katika uchaguzi wa rais tangu mwaka 1984.

Wisconsin inajulikana kwa viwanda vyake vya maziwa na jibini, ambavyo vimepigwa vibaya na sera za biashara za White House na janga la Covid-19, lakini kiwango cha msaada kwa wakulima cha dola bilioni 28 wiki kadhaa kabla ya kura hakikutarajiwa.

Rais Trump katika mkutano huo alimkosoa sana mpinzani wake kwa sera zake mbali mbali.

Trump akizungumza katika mkutano wa historia ya Marekani White House Septemba 17, 2020.
Trump akizungumza katika mkutano wa historia ya Marekani White House Septemba 17, 2020.

"Joe Biden ametumia Maisha yake yote ya kazi kusafirisha ajira za watu wa Wisconsin hadi nchi za nje, alihamisha ng'ambo makampuni yenu, ameruhusu mipaka yenu kuwa wazi, kukutumbukizeni katika vita visivyo na mwisho na kutoa muhanga mustakbal wa watoto wenu kwa China. "

Huku zikiwa zimesalia siku 46 kabla ya uchaguzi Trump yuko nyuma ya Biden katika majimbo saba muhimu yenye ushindani mkubwa kwa mujibu wa ukusanyaji maoni wa New York Times uliofanywa katika muda wa siku saba zilizopita.

Kwa mujibu wa uchunguzi huo rais hajaongoza katika jimbo hata moja kati ya hayo, na katika majimbo hajapata zaidi ya asilimia 44 ya kura. Ni muhimu kushinda majimbo hayo ili kumruhusu mgombea rais kushinda uchaguzi wa Novemba.

XS
SM
MD
LG