Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 16:19

Biden atakuwa Rais wa 46 wa Marekani


Rais mteule Joe Biden
Rais mteule Joe Biden

Makamu rais wa zamani wa Marekani Joe Biden, ambaye anajulikana katika siasa za Washington kwa karibu nusu karne, ametajwa kwamba atakuwa rais na anatarajiwa kuapishwa Januari 20, na kuwa rais mwenye umri mkubwa kuliko marais wote waliopita.

Biden Mdemokrat aliyehudumu kwa miaka 36 katika Baraza la Seneti la Marekani na miaka minane kama makamu wa Rais chini ya Rais wa zamani Barack Obama, ametangazwa na vyombo vya habari ikiwemo Sauti ya Amerika, Kuwa atamshinda Rais Mrepublikan aliyoko madarakani Donald Trump katika uchaguzi uliokuwa na ushindani mkali na baada ya siku kadhaa za kuhesabu kura baada ya uchaguzi kumalizika.

Matokeo yanasubiri kuthibitishwa rasmi na pia kutakuwa na changamoto ya kufikishwa mahakamani.

Biden ameshinda urais kwa kupata kura zisizopungua 270 kutokana na kura za Wajumbe 538.

Ushindi wa Biden utamfanya Trump kiongozi mkuu wa Marekani wa tatu katika miongo minne iliyopita kushindwa kuchaguliwa tena baada ya miaka minne ya uongozi wa taifa la Marekani.

Ushindi wa Biden umekuja siku kadhaa baada ya siku ya uchaguzi rasmi uliofanyika Jumanne wakati maafisa wa uchaguzi katika nusu dazeni ya majimbo kumaliza kuhesabu mamilioni ya kura zilizopigwa kwa njia ya posta zilizotumwa na wapiga kura ambao hawakufika katika vituo vya kupiga kura kwa kuhofia kupata maambukizi ya virusi vya corona.

Biden, atakuwa na umri wa miaka 78 siku ya kuapishwa, ameshinda nafasi ya urais baada ya kujaribu mara tatu kugombea baada ya kushindwa kupata uteuzi wa chama cha Demokratik kuwania nafasi hiyo mwaka 1988 na 2008, alipopata uungwaji mkono mdogo kwa miaka yote hiyo.

Rais mteule Joe Biden na Makamu Rais mteule Kamala Harris
Rais mteule Joe Biden na Makamu Rais mteule Kamala Harris

Hivi sasa ataongoza serikali ya Marekani akishirikiana na makamu wake wa rais ambaye ni mgombea mwenza, Seneta wa California Kamala Harris, mwanamke wa kwanza katika historia ya miaka 244 ya nchi hii kuchaguliwa kuwa rais au makamu wa rais.

Ni mtoto wa baba mwenye asili ya Jamaica na mama mwenye asili ya India na alikuwa ni mwanamke wa kwanza wa rangi katika tiketi ya siasa ya kitaifa Marekani.

Biden, baada ya kauli mbiu ya Trump “America First” (Marekani Kwanza) iliyopelekea kuiondoa Marekani katika mikataba ya kimataifa, ameahidi Marekani itarudi tena kushirikiana na ulimwengu, kujiunga ten ana mkataba wa mabadiliko ya hali ya hewa wa Paris na mkataba wa kuidhibiti Iran kutengeneza silaha za nyuklia.

Marekani inatumia njia isiyokuwa ya moja kwa moja kuunda demokrasia, siyo kwa kura za wananchi kitaifa, katika kuwachagua viongozi wake.

Matokeo ya uchaguzi yanaamuliwa jimbo kwa jimbo katika majimbo yote 50 nchini na mji mkuu wa Marekani, Washington, D.C.

Mshindi anahitaji kura za wajumbe 270 au zaidi kutoka kwa Wajumbe 538 wanaopiga kura.

XS
SM
MD
LG