Ndege moja ya jeshi nchini Angola imeanguka kati kati ya nchi hiyo na kuwauwa watu wasiopungua 30, wakiwemo majenerali watatu wa jeshi la Angola.
Taarifa kwa lugha ya kireno zinasema ndege hiyo imeanguka Jumatano wakati ikijaribu kuruka kutoka uwanja wa ndege katika mji wa kati kati wa Huambo. Ndege hiyo ya Angola Air Force ilitengenezwa na shirika la ndege la Brazil, ilikuwa imebeba ujumbe wa maafisa wa jeshi wa vyeo vya juu nchini Angola.
Watu wasiopungua sita wamenusurika katika ajali hiyo. Sababu za ajali hiyo bado hazijajulikana.