Serikali ya Uganda imetangaza mpango wa kuwahamisha watu laki tano kutoka maeneo ya hatari karibu na milima Elgon, Ruwenzori na Kigezi.
Waziri wa mipango ya dharura na majanga Saidi Musa Ecweru amesema zoezi hilo litaanza mara baada ya serikali kuwasilisha pendekezo lake mbele ya bunge na kupata maeneo muafaka ya makazi mapya ya wananchi kutoka maeneo hayo.
Hatua hii inatokana na maafa yaliyotokea wiki iliyopita kutokana na maporomoko ya ardhi yaliyosababisha vifo vya karibu watu 300, kulingana na maafisa wa serikali.
Akizungumza na Sauti ya Amerika Bw Ecweru ametoa wito kwa wananchi wa Uganda kushirikiana na serikali ili kukamilisha mpango huo badala ya kung’ang’ania kubaki katika maeneo yasiyo salama kwa maisha yao.
Changamoto kubwa kwa serikali ni kuweza kuwarai wakazi wengi wa maeneo hayo ya milimani,kuhama kwani wanadai kwamba ni mashamba yao na wameishi tangu enzi za mababu yao.
Maeneo mengi ya Uganda yamezungukwa na milima ambako misitu mikubwa imekatwa kutokana na kuongezeka idadi ya wananchi na haja ya kutafuta maeneo ya kilimo zaidi. Matokeo yake ni mmomonyoko wa ardhi na mafuriko wakati wa mvua.
Wakati huo huo, waziri Ecweru amesema takriban watu elfu nne walioathirika na maporomoko ya ardhi wiki iliyopita mashariki mwa Uganda wataanza kuhamishwa hivi karibuni kupelekwa katika makambi.