Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:39

Zaidi ya watu milioni 3 waathirika Haiti


Mashirika ya kimataifa ya kutoa msaada wa dharura duniani yalikuwa yanajitayarisha siku ya Jumatano kuanzisha msaada maalum kwa ajili ya Haiti kufuatia tetemeko kubwa la ardhi kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka 200.

Kufuatana na ripoti za vyombo vya habari kitovu cha tetemeko hilo lililokuwa na nguvu za 7.0 kwenye kipimo cha Richter lilitokea maili 10 kutoka mji mkuu wa Port-au-Prince na kuangusha majengo na miundo mbinu ya mawasiliano na umeme kutoka mji huo maskini wenye wakazi milioni 2.

Walinda amani wa UN, wengi wao kutoka Brazil wamekuwa wakijaribu kuwaokowa watu kutoka katika vifusi vya jengo la ghorofa tano.

Akionekana na huzuni alipokua anazungumza na waandishi wa habari, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon amesema zaidi ya watumishi 100 wa Umoja wa Mataifa hawajulikani waliko huko Haiti, na umoja huo unatathmini maafa na hasara zilizopatikana kutokana na tetemeko kubwa la ardhi, lililotokea jana jioni nchini humo. Katibu mkuu amesema anamtuma haraka afisa mmoja wa cheo cha juu huko Haiti na pia kutoa dola milioni 10 za msaada wa dharura.

Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa alisema tetemeko la ardhi limeharibu kabisa mji mkuu wa Port-au-Prince, lakini maeneo mengine ya nchi inaonekana hayajaathirika. Huduma za msingi kama vile maji na umeme katika mji mkuu zimekwama kabisa. Umoja wa Mataifa unazaidi ya walinda amani na polisi elfu tisa huko Haiti, pamoja na watumishi wa kiraia elfu moja na mia tisa. Makao makuu ya Umoja wa Mataifa katika hoteli ya Christopher yalianguka jana, lakini makao ya vyombo vyake muhimu hayakuharibika hata kidogo. Umoja huo unakhofia wafanyakazi wake, ambao hawajulikani walipo hadi hivi sasa huwenda wamenaswa ndani ya vifusi vya hoteli.

Huko Haiti raia walionekana kupanga maiti zilizopatikana kandokando ya barabara, na shirika la msalaba mwekundu huko Geneva linasema takriban watu milioni 3 wameathirika na tetemeko hilo kubwa lililokua na ngvu za 7.0 kwenye kipimo cha Richter. Shirika hilo linasema kunahitajika haraka watu watakoajitolea kufanya kazi za uwokozi kwenye hospitali na vituo vya afya vya dharura, pamoja na mfumo mpya wa kusafisha maji na mawasiliano.

MATAIFA DUNIANI KUISAIDA HAITI
Marekani na mataifa mengi ya kigeni yameshanza kupeleka msaada wa dharura huko Haiti, Rais Barack Obama ameahidi mpango kabambe wa dharura utakao ratibiwa vyema kusaidia Haiti. Akizungumza Jumatano alisema, timu za msaada wa dharura kutoka Marekani ziko njiani kuelekea Haiti, amesema picha kutoka Haiti ni za kusikitisha sana.
“Watu wa Haiti watapata uungaji mkono kamili wa Marekani kwa haraka kabisa kuwaokoa watu walionaswa ndani ya kifusi na tutawasilisha huduma za dharura, kama vile chakula, maji na dawa, kwa siku zinazokuja.”
Alisema timu ya uokoaji imeshaondoka na msaada zaidi uko njiani. Na alieleza bayana hakuna wakati wa kupoteza hivi sasa.


Ufaransa, Italy, Uingereza na Brazil pia zimeanza kupeleke timu za uokoaji na wasaidizi.
Idara ya chakula duniani-WFP, imesema inasafirisha chakula kwa ndege kutoka ghala zake huko El Salvador, msaada huo unaweza kuwapatia chakula zaidi ya watu nusu milioni.

XS
SM
MD
LG