Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 28, 2025 Local time: 01:15

AU walaani mashambulizi Somalia


Umoja wa Afrika umelaani vikali shambulizi la bomu la kujitoa mhanga nchini Somalia ambalo limeua walinzi wa amani tisa wa umoja huo, ikiwa pamoja na naibu kamanda wa kikosi hicho. Kundi la kiislamu lenye msimamo mkali lilisema lilifanya shambulizi hilo kwenye uwanja wa ndege wa Mogadishu kulipiza vifo vya viongozi wao.

Mwenyekiti wa tume ya Umoja wa Afrika Jean Ping, alitoa heshma kwa walinzi wa amani waliouawa, katika mkutano na waandishi wa habari. Aliwaelezea washambuliaji kuwa ni wahalifu wenye mienendo ya kigaidi wenye azma ya kuhujumu maendeleo yaliyopatikana katika miezi ya karibuni, ya kutafuta suluhisho la kudumu la vita vya karibu miongo miwili nchini Somalia.

Taarifa iliyotolewa baadaye iliita shambulizi hilo ni ushahidi wa tishio linaloletwa na makundi ya kihalifu na kigaidi na wafuasi wao, wote walio ndani na nje ya Somalia.

Maafisa wa Umoja wa Afrika wamesema miongoni mwa waliouwawa ni pamoja na Meja Jenerali Juvenal Niyoyunguruza wa Burundi, ambaye ni naibu kamanda wa kikosi cha walinzi wa amani elfu 5, wajulikano kama AMISOM. Kamanda wa juu kutoka Uganda, Jenerali Nathan Mugisha wa Uganda, alikuwa miongoni mwa wale waliojeruhiwa.

Mashahidi wamesema milipuko ilikuwa imefichwa katika magari mawili yaliyokuwa na nembo ya Umoja Mataifa, ambayo yaliruhusiwa na walinzi wa amani kuingia eneo la uwanja wa ndege wa Mogadishu.

Kundi la waasi wa kiislamu wenye msimamo mkali, wamedai kuhusika. Msemaji wa waasi, amesema shambulizi lilikuwa ni majibu kwa operesheni za kijeshi za Marekani zilomuua mshukiwa wa ugaidi mwenye uhusiano na Al Qaida Jumatatu kusini mwa Somalia.

Maafisa wa Marekani wamesema mshukiwa alikuwa akitafutwa na Shirika la Upelelezi la Marekani - FBI - kwa shambulizi la bomu la mwaka 2002, kwenye hoteli moja iliyokuwa inamilikiwa na Israel huko mjini Mombasa, Kenya.

XS
SM
MD
LG