Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 03:31

Zoezi la sensa Kenya linaendelea bila matatizo makubwa.


Zoezi la kuhesabu watu nchini Kenya limeendelea jumanne kwa siku ya pili mfululizo. Pia leo imekuwa siku ya mapumziko nchini humo ili kutoa nafasi kwa watu wengi kushiriki kwenye zoezi hilo la sensa. Lakini bado kuna idadi kubwa ya watu ambao hawajahesabiwa hadi hivi sasa.

Shughuli hizi zimekuwa zikiendelea kwa amani lakini kwa taratibu sana. Katika maeneo kadhaa mjini Nairobi, Mombasa na mikoa ya Kati na Magharibi kumekuwa na visa vidogo vidogo vya kutatiza shughuli hizo, lakini serikali iliweza kuyatanzua matatizo hayo.

Katika mkoa wa Kati, vijana kadhaa wafuasi wa kundi haramu la Mungiki, walikamatwa na polisi walipokuwa kwenye sherehe za kula viapo na wengine walipatikana na silaha za kitamaduni. Huko mjini Mombasa baadhi ya maafisa wa zoezi hizo waliendelea kulalamika kuhusu tatizo la malipo.

Na katika mtaa wa Soweto mjini Nairobi baadhi ya maafisa wa zoezi walifukuzwa na raia baada ya kukosa vitambulisho. Na katika kisiwa cha Migingo kinachokabiliwa na mzozo kati ya Kenya na Uganda hali ilikuwa shwari. Lakini katika maeneo ya Kaskazini Mashariki wakazi wengi wa maeneo hayo hawakuweza kuhesabiwa kwasababu walikuwa tayari wameshahma kutoka nyumba zao kutafuta malisho ya mifugo kutokana na hali mbaya ya ukame. Lakini kwa ujumla tatizo kubwa katika zoezi hilo ilikuwa ni hali ya usalama.

XS
SM
MD
LG