Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 18, 2024 Local time: 17:47

Matibabu yafanyika kwenye korido za hospitali huko Sudan


Wodi iliyojaa majeruhi katika hospitali ya El Fasher katika eneo la Darfur Kaskazini tarehe 21, 2023. Picha na Ali SHUKUR / Médecins sans Frontières (MSF) / AFP.
Wodi iliyojaa majeruhi katika hospitali ya El Fasher katika eneo la Darfur Kaskazini tarehe 21, 2023. Picha na Ali SHUKUR / Médecins sans Frontières (MSF) / AFP.

Watoto walipigwa risasi na wagonjwa walitibiwa kwenye korido: hizi ni ripoti za mwanzo kutolewa na madaktari tangu mapigano yalipozuka nchini Sudan ikionyesha hali ya kutisha na athari za "kubwa" za mzozo huo.

Ushuhuda huo, uliotolewa na Cyrus Paye, ambaye ni mfanyakazi wa Shirika la Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) katika mkoa wa Darfur uliokumbwa na vita, ulionyesha picha ya kutisha kuhusu ghasia zilizozuka katika maeneo mbalimabli kote nchini mwishoni mwa wiki.

"Wengi waliojeruhiwa ni raia ambao walipigwa risasi zilizofyatuliwa kiholela, waathirika wengi ni watoto," Paye alisema, mratibu wa mradi wa MSF katika Hospitali ya Kusini huko El Fasher, mji mkuu wa Darfur Kaskazini.

"Watu walikuwa wamevunjika kwa kupigwa risasi, au wana majeraha ya risasi au wana vipande vya risasi kwenye miguu yao, tumboni au kifuani. Wengi wanahitaji kuongezewa damu."

Hospitali ya Kusini inayopata msaada kutoka MSF kwa kawaida ni kitengo cha uzazi ambacho hakina uwezo wa kufanya upasuaji, lakini madaktari walipaswa kuchukua hatua za haraka.

"Tangu mapigano yalipoanza, tumelazimika kubadilisha malengo ya hospitali ili kuweza kuwatibu majeruhi," Paye alisema.

"Hali ni mbaya sana," Paye alisema.
"Kuna wagonjwa wengi ambao wanatibiwa wakiwa sakafuni kwenye korido kwa sababu hakuna vitanda vya kutosha kutosheleza idadi kubwa ya majeruhi," aliongeza.

Hospitali nyingine mjini humo zimelazimika kufungwa, huku hospitali ya watoto "imeporwa kila kitu", Paye alisema.

Madaktari kutoka katika hospitali hizo wamekuja kusaidia katika Hospitali ya Kusini, lakini foleni ya wagonjwa inaendelea kuongezeka.

Chanzo cha habari hii ni shirika la habari la AFP.

XS
SM
MD
LG