Wito huo ulitolewa wakati wa maandamano makubwa yaliyofanyika kote nchini yaliyoitishwa na kanisa hilo, ili kulalamika dhidi ya ghasia zinazoendelea mashariki ya nchi hasa katika maeneo ambayo wapiganaji wa kundi la M23 wanashikilia.
Wakibeba tasbihi, mabango na Biblia, waandamanaji wa rika zote walishuka katika njia za miji mbali mbali kwa maandamano yaliyofanyika katika takriban mitaa 15 ya mji mkuu wa Kinshasa, pamoja na miji mingine ya Congo.
Waandamanaji walikua wanaimba nyimbo za kidini wakisema "Hatutaki nchi yetu kukaliwa," "Hatutaki tena unafiki unaofanywa na Jumuia ya Kimataifa" na "tuna laani mtu au nchi yeyote inayotushambulia."
Maandamano ya mjini Goma yaliahirishwa kwa hofu ya kuingiliwa kati na waasi.
Hali ya utulivu hata hivyo imeripotiwa Jumapili ingawa kuna baadhi ya vyanzo vinaripoti kwamba wapiganaji wa M23 wamekua wakijiimarisha, wakionekana wanaelekea katika kijiji cha Kishishe.