Wanamgambo wa kundi la M23 wamekuwa wakipata nguvu zaidi tangu walipoanzisha mashambulizi katika jimbo la Kivu Kaskazini mapema mwaka huu, na wako umbali wa kilomita chache tu kutoka Goma, jiji lenye takriban watu milioni 1.
Mapigano hayo yamesababisha kuongezeka kwa mvutano wa kidiplomasia na nchi jirani ya Rwanda, ambayo Kongo, inaituhumu kuwaunga mkono waasi, mashtaka ambayo Kigali inakanusha.
Siku ya Jumatano, hata hivyo, mazungumzo kati ya nchi hizo mbili katika mji mkuu wa Angola, Luanda, yalipelekea kile kilichoelezwa kuwa makubaliano ya "kusitisha mapigano mara moja," kuanzia leo Ijumaa.
Pande zote mbili pia, zilikubaliana kuhusu haja ya "kuondolewa mara moja" kwa kundi la M23 "kutoka maeneo linayoyakalia."
Onesphore Sematumba, mchambuzi wa Taasisi ya ya Migogoro ya Kimataifa, alisema ukweli kwamba mkutano huo ulisimamiwa na Angola, ilikuwa ni ishara njema, "kutokana na kuongezeka kwa mvutano."
Lakini wengine walihoji ni kwa nini waasi hawakushiriki. Pia walihoji ni kwa nini Rais wa Rwanda Paul Kagame, pia hakuwepo.
Jean-Claude Bambaze, ambaye anaongoza mashirika ya kiraia katika eneo la Rutshuru, ambalo sehemu zake zimetekwa na M23, alisema anatumai waasi hao sasa watajiondoa. Lakini, aliongeza, "tuna wasiwasi, kwa sababu haitakuwa mara ya kwanza kwa maamuzi ya kisiasa kutotekelezwa."