Waandamanaji wawili waliuawa kwa kupigwa risasi wakati wa maandamano nchini Sudan siku ya Alhamis huku maafisa wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika wakionya kuwa nchi hiyo iko hatarini.
Mamia ya waandamanaji waliingia kwenye mitaa yote ya Khartoum na mji wake pacha wa Omdurman, mashahidi walisema. Vikosi vya usalama vilimpiga risasi na kumuuwa muandamanaji mmoja huko Omdurman na mwingine mjini Khartoum, madaktari wanaounga mkono demokrasia walisema.
Takribani watu 87 wameuawa na mamia kujeruhiwa wakati wa zaidi ya miezi minne ya maandamano ya kudai utawala wa kiraia na haki kwa wale waliouawa katika maandamano ya awali kulingana na madaktari.
Viashiria vyote vinavyopatikana kwetu katika umoja wa Mataifa na AU vinaonyesha kuwa nchi iko kwenye hatari kubwa alisema mjumbe wa Umoja wa Afrika, Mohamed Lebatt katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari mjini Khartoum akiwa na mwakilishi maalum wa UN, Volker Perthes.
“Tuna wasiwasi mkubwa kuhusu hali ya nchi alisema akitoa wito wa kuanza upya kwa utawala kamili wa kiraia”. AU imesimamisha uanachama wa Sudan tangu mkuu wa jeshi Abdel Fattah al-Burhan kuongoza mapinduzi ya Oktoba mwaka 2021.