Vikosi vya usalama vya Sudan vilimkamata kiongozi mkuu wa upinzani hapo Jumanne huku maafisa wakifyatua gesi ya kutoa machozi kuwazuia maelfu ya waandamanaji waliokuwa wakiandamana kupinga mapinduzi ya kijeshi ya mwaka 2021 mwandishi wa shirika la habari la AFP alisema.
Maandamano hayo yalikuwa ya hivi karibuni tangu jeshi lilipochukua madaraka Oktoba 25 mwaka 2021 yaliyoongozwa na mkuu wa jeshi Abdel Fattah al-Burhan ambayo yalifuatiwa na msako mkali dhidi ya raia na watu wanaounga mkono demokrasia katika taifa hilo la kaskazini-mashariki mwa Afrika.
Takribani watu 85 wameuawa na mamia kujeruhiwa na vikosi vya usalama wakati wa zaidi ya miezi minne ya maandamano ya kudai utawala wa kiraia na haki kwa wale waliouawa katika maandamano kulingana na madaktari.
Siku ya Jumanne vikosi vya usalama vilifyatua gesi ya kutoa machozi kwa umati wa watu waliokuwa wakielekea makazi ya rais huku watu kadhaa walijeruhiwa mwandishi wa AFP alisema. Baraza la utawala lina makao yake katika ikulu, kando ya mto Nile mjini Khartoum.
Maandamano ya Jumanne yalienda sambamba na siku ya kimataifa ya wanawake. Umati wa watu uliimba nyimbo za kuunga mkono wanawake wa Sudan ambao wamekuwa na jukumu muhimu katika vuguvugu la hivi karibuni la maandamano na pia katika mikutano iliyofungua njia kuelekea kuondolewa madarakani kwa kiongozi wa muda mrefu nchini Sudan Omar al-Bashir hapo mwaka 2019.