Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 06:44

Jeshi la Uganda laapa kusambaratisha ADF kwa kila namna


Jeshi la Uganda limesema kwamba litafanya kila liwezekanavyo kuhakikisha kwamba waasi wa Allied democratic forces hawatumii maficho yao katika jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kama kituo cha kimkakati kueneza ugaidi katika nchi za Afrika mashariki na maziwa makuu.

Akizungumza na Sauti ya Amerika kwa njia ya simu, msemaji wa jeshi la Uganda UPDF Brig. Flavia Byekwaso, amesema kwamba kufikia sasa, mashambulizi ya jeshi la Uganda dhidi ya waasi wa ADF ndani ya DRC, yamefikia malengo na kulipua sehemu 4 zilizolengwa katika mashambulizi ya makombora ya awali yaliyovurumishwa kutoka Uganda.

Amesema kwamba hakuna raia ameuawa wala kujeruhiw akatika mashambulizi hayo.

“Huu ni mwanzo wa mwisho wa ADF. Hatutawaacha waasi wa ADF hadi tutakapoharibu kabisa maficho yao na kuwaua. Ni lazima tumalize hii shida ya ugaidi unaofanywa na ADF. Wanajificha Congo na wanakuja Uganda kuua watu. Wanaua watu Congo” amesema Byekwaso, akiongezea kwamba “tuliwafukuza Uganda na wakaenda kujificha Congo. Tumewafuata huko. Lazima tukabiliane nao na kumaliza nguvu yao”.

Mwandishi wa Sauti ya Amerika Austere Malivika, amesema kwamba wanajeshi wa Uganda wamepiga hatua kadhaa ndani ya DRC na wanaendelea na mashambulizi.

Bunge la Uganda limekosoa hatua ya jeshi la nchi hiyo kuingia DRC bila idhini ya bunge. Lakini msemaji wa jeshi Brigedia Byekwaso amesema kwamba “rais ana mamlaka ya kutuma wanajeshi nchi Jirani au kwa maslahi ya taifa bila idhini ya bunge na analostahilikufanya ni kumwandikia barua spika wa bunge akimweleza kuhusu hatua yake”.

Kambi za waasi wa ADF za Madina 1 na 2 Kivu kaskazini, Pamoja na Katanda na mashini, zinaripotiwa kuharibiwa na makombora ya jeshi la Uganda.

XS
SM
MD
LG