Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatatu, Machi 24, 2025 Local time: 00:25

Kenyatta aapishwa: Afungua mipaka ya Kenya kwa Afrika Mashariki


Rais Uhuru Kenyatta akionesha hati ya kuchukua madaraka kwa awamu ya pili, uwanja wa Kasarani Nairobi.
Rais Uhuru Kenyatta akionesha hati ya kuchukua madaraka kwa awamu ya pili, uwanja wa Kasarani Nairobi.

Rais Uhuru Kenyatta ameapishwa mjini Nairobi leo kuchukua awamu ya pili ya uongozi wa Kenya baada ya kushinda uchaguzi wa marudio wa Oktoba 26.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na maelfu kwa maelfu ya Wakenya katika uwanja wa Kasarani. Viongozi tisa wa nchi za nje walihudhuria sherehe hizo ikiwa ni pamoja na marais Yoweri Museveni wa Uganda, Seretse Ian Khama wa Botswana.

Rais Kenyatta anakabiliwa na kazi ngumu ya kuwaunganisha Wakenya baada ya uchaguzi ulioigawa nchi hiyo, na pia kuinua uchumi ambao ulidorora katika kipindi cha uchaguzi.

Ndugu zetu wa Afrika Mashariki

Katika hotuba yake ya ufunguzi Rais Kenyatta alitangaza kuwa kuanzia sasa raia wa Afrika Mashariki watachukuliwa kama Wakenya katika nchi hiyo. Alisema kwa kutumia tu kitambulisho cha uraia wa nchi ya Afrika Mashariki mtu anaweza kufanya kazi, kumiliki mali, shamba, kuoa na kuolewa na kuishi nchini Kenya.

Kenyatta aliongeza kuwa serikali yake imechukua hatua hiyo bila ulazima wa nchi nyingine za Afrika mashariki kufanya hivyo hivyo.

Hii ni hatua kubwa sana katika uhusiano wa nchi za shirikisho la Afrika mashariki - Kenya, Tanzania, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini - ambazo zimekuwa zikijaribu kuondoa vikwazo vingi katika maisha ya kawaida ya wananchi wao bila mafanikio makubwa.

Usafiri, biashara na ukazi miongozi mwa nchi hizo bado ni kikwazo katika muingiliano wa nchi hizo licha ya kwamba shirikisho hilo limedumu kwa miaka mingi.

XS
SM
MD
LG