Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 13:23

Chadema yamuomba Magufuli kumtathmini waziri wa mambo ya ndani


Rais Magufuli
Rais Magufuli

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimemuomba Rais John Magufuli kutafakari upya kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, bado anafaa kuongoza Wizara hiyo, kufuatia wimbi la matukio yanayoashiria ukosefu wa usalama nchini.

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema), amedai kuwa “Waziri wa Mambo ya Ndani, tangu Tundu Lissu ameshambuliwa hajawahi kurusha hata mguu Nairobi, hata kwenda kuongea na Waziri wa Mambo ya Ndani Kenya, kuomba ulinzi kwa ajili ya mgonjwa.”

“Wakati ni mbunge mwenzake, tena wa mkoa wake amepigwa risasi, Mwigulu Nchemba hajajishughulisha na janga lililompata Lissu na anaongea vitu vyepesi kuhusu maisha ya watu.”

Lema, ambaye ni waziri kivuli wa wizara hiyo, alisema hayo jana, wakati akizungumzia kauli za Mwigulu kuhusu kupigwa risasi kwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) na matukio mengine, yakiwamo ya kupotea kwa aliyekuwa msaidizi wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Ben Saanane.

"Kwa kauli zake kama kuna mtu alimtazama wakati anaongea, utajua tukio la Lissu limefanywa na nani, na nani yuko nyuma ya tukio hili, vinginevyo angekuwa na ujasiri wa kuelekeza polisi kutafuta wahalifu kwa nguvu zote, angewaza pengine anayefuata ni yeye,” aliongeza.

“Serikali ijue tu kama tukio hili la Lissu haliko “connected” na wao, waliofanya tukio hili wana nia mbaya,” alisema Lema.

“Nilifikiria Mwigulu angeachana na ngonjera zake akaongelea habari angalau ya maslahi ya askari, Mwigulu amenisikitisha sana, na sidhani kama anastahili kukaa kwenye ile ofisi hata kwa saa mbili," ameongeza Lema.

Chadema hivi karibuni imeibua maswali kuhusiana na kauli za serikali ya Tanzania, wakisema ndiyo sababu wanataka uchunguzi wa kupigwa risasi Mbunge Tundu Lissu ufanywe na vyombo vya upelelezi vya kimataifa.

Baadhi ya maswali yaliyoibuliwa na Chadema ni pamoja na vipi serikali ilijua gari ambalo Lissu alisema lilimfuatilia akiwa Dar halijawahi kufika Dar es Salaam, ili hali nchi haina kamera barabarani wala kwenye mitaa.

Pia kimehoji ni kwa namna gani Waziri wa Mambo ya Ndani anasema magari yanayofanana na lililokuwa limebeba watu waliomshambulia Lissu yamekamatwa 10, huku kukiwa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusika na shambulio hilo.

Chadema inadai ni mkanganyiko kama aliouibua Mwigulu Nchemba, ndiyo unaofanya itake suala hilo lichunguzwe na vyombo vya nje ya nchi.

XS
SM
MD
LG