Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 03, 2024 Local time: 21:22

Trump ajisalimisha katika jela ya kaunti ya Fulton, aachiliwa kwa dhamana


Picha ya rais wa zamani wa Marekani Donald Trump iliyopigwa katika jela ya kaunti ya Fulton alipojisalimisha Agosti 24, 2023.
Picha ya rais wa zamani wa Marekani Donald Trump iliyopigwa katika jela ya kaunti ya Fulton alipojisalimisha Agosti 24, 2023.

Rais wa zamani wa Marekani, Donald Trump, Alhamisi jioni aliwasili katika jela ya kaunti ya Fulton katika mji wa Atlanta, jimbo la Georgia, ambako alijisalimisha kufuatia kufunguliwa mashtaka dhidi yake na wengine, kwa kujaribu kubadili matokeo ya uchaguzi wa 2020, na uhalifu mwingine.

Trump, ambaye aliachiliwa kwa dhamana, na kuondoka muda mfupi baadaye, alishtakiwa mapema mwezi huu kwa kukiuka sheria za jimbo la Georgia za ubadhirifu na "kutenda uhalifu mwingine, akikbiliwa na mashtaka 13 katika jimbo la Georgia."

Alhamisi, alichukuliwa alama za vidole na picha yake akiwa jela, maarufu kama Mug Shot, ikapigwa, wasaidizi walisema.

Hakuna rais mwingine wa zamani wa Marekani ambaye ameshtakiwa kwa makosa ya jinai, lakini Trump sasa anakabiliwa na kesi nne, na jumla ya mashtaka 91 kwa madai ya vitendo vyake vya kabla, wakati na baada ya muhula wake mmoja wa urais uliomalizika mwaka 2021.

Washtakiwa wengine, akiwemo wakili wake wa zamani Rudy Giuliani, wamejisalimisha kwenye jela kwa muda wa siku chache zilizopita.

Trump alikuwa katika jela ya kaunti ya Fulton kwa takriban dakika 20.

Nje ya jela ya kaunti ya Fulton, Georgia, ambako rais wa zamani wa Marekani Donald Trump alijisalimisha.
Nje ya jela ya kaunti ya Fulton, Georgia, ambako rais wa zamani wa Marekani Donald Trump alijisalimisha.

Baadaye aliwahutubia waandishi wa habari kwa muda mfupi katika uwanja wa ndege wa Hartsfield Jackson, ambapo alisema hajatendewa haki.

"Nina uhuru wa kupinga matokeo ya uchaguzi," alisema, kabla ya kwelekea kwa ndege yake.

Mapema wiki hii, Trump alikubali dhamana ya dola 200,000 na masharti mengine ya kuachiliwa, ikiwa ni pamoja na kutotumia mitandao ya kijamii kuwatisha washtakiwa wenzake au mashahidi katika kesi hiyo.

Hii ndiyo kesi ya kwanza ambapo Trump ametakiwa kulipa dhamana ya pesa taslimu. Uwezekano wake wa kuachiliwa bila dhamana ya pesa taslimu ulikuwa mdogo huko Georgia.

Trump alikuwa tayari anakabiliwa na mashtaka mengine matatu ya uhalifu alipofunguliwa mashtaka hayo mapya.

Forum

XS
SM
MD
LG