Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Mei 02, 2024 Local time: 22:26

Korea Kusini, China zakubaliana kulikabili tishio la Pyongyang


Manuari ya Marekani USS Carl Vinson wakifanya matayarisho ya kupakia makombora kabla ya kuanza patroli ya eneo la South China Sea
Manuari ya Marekani USS Carl Vinson wakifanya matayarisho ya kupakia makombora kabla ya kuanza patroli ya eneo la South China Sea

Korea Kaskazini na China wamesema wamekubaliana watachukua hatua kali dhidi ya Korea Kaskazini iwapo Pyongyang itafanya majaribio zaidi ya nyuklia na makombora ya ballistiki yanayofika sehemu yoyote duniani.

Wawakilishi wa ngazi ya juu wa masuala ya Nyuklia kutoka kwa majirani zake Korea Kaskazini, Kim Hong-kyun na Wu Dawei, wamejadiliana matukio ya hivi karibuni Jumatatu huko mjini Seoul.

Jumapili, Mshauri wa Usalama wa Taifa wa Marekani HR McMaster amesema Rais Donald Trump amewataka maafisa kumpa mapendekezo mbalimbali kama hatua ya kuondosha hatari ya silaha za nyuklia zinazomilikiwa na Korea Kaskazini.

Wakati kikundi cha Jeshi la Majini la Marekani kimeelekea huko rasi ya Korea ilikutoa ujumbe kwa Korea Kaskazini, McMaster ameiambia Fox News, “Huu (Korea Kaskazini) ni utawala wa kidikteta ambao sasa umeshamiliki silaha za nyuklia.

…Kwa hiyo rais ametuagiza sisi kujitayarisha kumpa mapendekezo mbalimbali ya kina kuiondoa hiyo hatari kwa watu wa Marekani na washirika wetu na wadau katika eneo hilo.”

McMaster ameeleza uamuzi wa Marekani kupeleka kikundi cha mashambulizi cha manuari ya Carl Vinson Strike kulinda maslahi ya Marekani katika upande wa Magharibi ya bahari ya Pacific ni “cha busara.”

Amesema kuwa Rais Trump na Rais wa China Xi Jinping wamekubaliana katika mkutano wao uliofanyika Florida wiki iliopita kuwa “tabia ya uchokozi” ya Pyongyang katika kutengeneza silaha za nyuklia haikubaliki.

“Marais kabla ya hapo na Rais Trump wanakubaliana hili halikubaliki, na kinachotakiwa kufanyika ni kuondosha silaha za nyuklia katika rasi hiyo,” amesema McMaster.

Msemaji wa Wizara ya Ulinzi wa Korea Kusini amesema Jumatatu kupelekwa kwa manuari ya Carl Vinson katika eneo la Magharibi la bahari ya Pacific ilikuwa kukabiliana na “hali ya hatari iliyoko katika rasi ya Korea.”

Moon Sang-gyun amesema inaeleweka kwamba Marekani na Korea Kusini wanafanya “maandalizi kamili kwa kuwepo uwezekano wa Korea Kaskazini kufanya vitendo vya uchokozi, ikizingatiwa kuwepo uwezekano wa mkakati wa Pyongyang wa kiuchokozi, pamoja na kuongezeka kwa nchi hiyo kufanya majaribio ya nyuklia na makombora.”

Korea Kaskazini imekuwa ikijaribu kutengeneza makombora ya masafa marefu yenye kubeba vichwa vya nyuklia ambavyo vinaweza kufika Marekani, umbali wa kilomita 8,000. Mpaka sasa imefanya majaribio ya nyuklia matano na inawezekana iko njiani kufanya jaribio la sita.

XS
SM
MD
LG