Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 03, 2024 Local time: 22:13

Marekani yawawekea vikwazo watu binafsi na makampuni "yanayofadhili al-Shabaab"


Wapiganaji
Wapiganaji

Afisi ya Wizara ya Fedha ya  Marekani inayohusika na Udhibiti wa Mali za Kigeni (OFAC), Jumatatu imeyawekea vikwazo mashirika 16 na watu binafsi, ambao inasema wanahusika katika mtandao mpana wa biashara unaozunguka Pembe ya Afrika, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Cyprus.

Imesema mtandao huo huchangisha na kutakatisha fedha, za kufadhili shughuli za wanamgambo wa al-Shabaab, kundi la kigaidi lenye mafungamano na al-Qa'ida.

Afisi hiyo inasema watu binafsi ndani ya mtandao huo ni pamoja na wafanyabiashara wenye ushawishi mkubwa katika eneo hilo ambao hutoa msaada wa kifedha kwa al-Shabaab, kikundi kilichohusika na baadhi ya mashambulizi mabaya zaidi ya kigaidi katika historia ya Afrika Mashariki.

Makapuni hayo ni pamoja na ile ya basi iitwayo Crown Bus Service ya Kenya, Haleel Comodities LLC na Qemat Al Najah General Trading. Wafanyabiashara waliolengwa ni pamoja na Faysa Yususfu Dini anayeishi nchini Kenya, Hassan Farah Mohamed na Mohamed Jumale Ali Awale.

“Mashambulizi haya yamesababisha vifo vya maelfu ya raia wasio na hatia. Watu hawa wanawekewa vikwazo kwa mujibu wa Agizo la Utendaji (E.O.) 13224, kama linalo makundi ya kigaidi na viwezeshaji vyao,” ilisema taarifa ya wizara hiyo.

"Marekani imejitolea kufanya kazi na washirika wa kikanda ili kung'oa mitandao ya ufadhili wa ugaidi na mashirika wanayotumia vibaya, kutafuta na kuhamisha fedha," alisema naibu wa waziri wa wizara ya fedha, anayehusika na masuala ya Ugaidi na Ujasusi wa Fedha Brian E. Nelson.

"Hatua ya leo ni sehemu ya juhudi nyingi za Wizara ya Fedha kuunga mkono juhudi za serikali ya Somalia dhidi ya al-Shabaab-moja ya nguzo tatu katika kampeni yao ya kudhalilisha kundi hili baya la kigaidi."

Al-Shabaab hupata zaidi ya dola milioni 100 kwa mwaka kwa kuwanyang'anya wafanyabiashara wa ndani na watu binafsi, na pia kupitia usaidizi wa kifedha wa wafanyabiashara washiriki, kwa mujibu wa wizara hiyo.

Marekani ilisema kwamba tishio linaloletwa na al-Shabaab haliko Somalia pekee. Mapato ya Al-Shabaab yanatolewa kwa vikundi vingine vinavyoungwa mkono na al-Qa'ida duniani kote na kusaidia kufadhili mipango ya al-Qa'ida ya kimataifa ya kuzusha mifarakano na kudhoofisha utawala bora.

Hatua hii inaendelea na juhudi za Marekani za kuvuruga matumizi ya al-Shabaab ya mfumo wa kifedha wa kikanda, na ni mwendelezo wa hatua za afisi ya OFAC ya Oktoba 2022, kuorodhesha mtandao wa wawezeshaji wa kifedha wa al-Shabaab ambao ilisema walitumika kama wajumbe wakuu wa majadiliano kati ya al-Shabaab na biashara za ndani nchini Somalia.

Forum

XS
SM
MD
LG