TANESCO yadai uhaba wa maji na mitambo mibovu kuwa chanzo cha mgao wa umeme Tanzania

fundi umeme akifanya matengenezo katika nguzo ya umeme

Masuala ya matengenezo na uhaba wa maji kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa yanasababisha upungufu wa umeme wa megawati 400 nchini Tanzania, na hivyo kupelekea mgao wa umeme katika taifa hilo la Afrika Mashariki, shirika la serikali ya kusambaza umeme limesema.

Gridi ya Taifa ya Tanzania, ambayo ina uwezo wa kuzalisha umeme wa zaidi ya MW 1,900 umeathiriwa na kuvunjika kwa miundombinu kwenye visima vya gesi na vituo vya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi, pamoja na kupungua kwa viwango vya maji katika mabwawa yanayozalisha umeme, amesema Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Gissima Nyamo-Hanga

TANESCO, ambayo inamilikiwa na serikali, inatarajia kukamilisha matengenezo na kutatua matatizo ya upungufu wa umeme ifikapo mwishoni mwa mwezi Machi mwakani, Nyamo-Hanga aliwaambia waandishi wa habari Jumatano jioni.

Licha ya serikali kuanzisha moja ya harakati kubwa za usambazaji wa umeme Afrika kusini mwa Jangwa la Sahara, ni asilimia 38 tu ya Watanzania wana umeme, kwa mujibu wa Benki ya Dunia.

Takriban theluthi mbili ya umeme wa Tanzania unazalishwa kutokana na gesi asilia, na takribani asilimia 30 ya umeme unatokana na nguvu ya maji. Mahitaji makubwa ya umeme kuwahi kurekodiwa yalikuwa MW 1,431 mwezi Mei mwaka huu, ikiwa ni asilimia saba kutoka mwaka jana, wizara ya nishati inasema.

"Tunatarajia kuwa shida hii itaanza kupungua ndani ya kipindi cha wiki mbili, mpango wetu ni kupunguza uhaba kwa wastani wa 100 MW kwa mwezi," Nyamo-Hanga alisema.

Bwawa la kufua umeme la MW 2,115 la Julius Nyerere lilianza kujazwa maji mwezi Desemba mwaka jana na kazi hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2024, zaidi ya mara mbili uwezo wa uzalishaji, kulingana na wizara ya nishati.

Serikali inajishughulisha na miradi mingine kadhaa ya umeme ikijumuisha shamba la sola la MW 150 ikiwa ni sehemu ya lengo lake la kufikia MW 5,000 ifikapo mwaka 2025.

Nyamo-Hanga alisema bwawa la Nyerere limekamilika kwa asilimia 92, lakini mabadiliko ya hali ya hewa yanasababisha uhaba wa mvua na kupunguza viwango vya maji katika mabwawa yaliyopo.

Chanzo cha habari hii ni shirika la habari la Reuters