Israeli yaidhinisha ujenzi wa makazi ya walowezi kwenye Ukingo wa Magharibi

Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu

Israel imeidhinisha ujenzi ambao umekuwa ukiendelea, wa makazi tisa ya walowezi wa kiyahudi, kwenye Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kimabavu.

Ujenzi mkubwa wa nyumba za Waisraeli katika makazi hayo pia utakuwa sehemu ya mpango huo.

Makazi mapya yaliyoidhinishwa huenda yakawa kikwazo kwa mapatano ya amani kati ya Palestina na Israeli, kwa sababu makazi ya walowezi yapo kwenye ardhi ambayo Wapalestina wanataka liwe taifa lao.

Wengi katika jumuiya ya kimataifa wanayachukulia makazi hayo kuwa haramu. Uidhinishaji huo ni moja ya hatua za kwanza za serikali ya Waziri Mkuu aliyechaguliwa tena, Benjamin Netanyahu.

Mashambulizi ya hivi karibuni yaliyotokea mashariki mwa Jerusalem inayokaliwa kwa mabavu yamesababisha vifo vya takriban Waisraeli 10.

Wakati huo huo, maelfu ya Waisraeli waliandamana nje ya bunge leo Jumatatu, kupinga mpango wa serikali wenye utata, wa mageuzi katika mfumo wa mahakama, ambao unalenga kuwapa wabunge udhibiti zaidi wa mahakama ya juu zaidi nchini humo.