Senegal imewazika watoto wachanga 11 waliokufa kwa ajali ya moto hospitalini

Wageni wakiwa nje ya jengo la hospitali ya Mame Abdoul Aziz Sy Dabakh kwenye mji wa Tivaouane, Senegal, May 26, 2022.

Senegal hapo Jumapili ilifanya mazishi ya watoto 11 ambao walikufa kutokana na moto uliowaka kwenye jengo la hospitali, Meya wa eneo hilo alisema baada ya mkasa huo kuibua hasira mpya juu ya hali ya mfumo wa afya.

Moto uliozuka Jumatano jioni katika mji wa magharibi wa Tivaouane ulikuwa wa hivi karibuni katika mfululizo wa vifo vya hospitali ambavyo vimefichua udhaifu wa mfumo wa afya wa Senegal.

Rais wa Senegal Macky Sall siku ya Alhamis alimfukuza kazi waziri wake wa afya lakini kwa wa-Senegali wengi hiyo haitoshi na wanaogopa majanga zaidi kutokea katika siku zijazo.

Mwezi uliopita mwanamke mjamzito alikufa kwa uchungu baada ya kuomba afanyiwe upasuaji lakini alikataliwa katika hospitali ya umma katika mji wa kaskazini-magharibi wa Louga.

Watoto 11 waliofariki katika ajali ya moto siku ya Jumatano kwenye wadi ya watoto wachanga walizikwa baada ya sala ya pamoja kwenye makaburi ya Tivaouane kulingana na matakwa ya familia zilizopoteza wapendwa wao. Mazishi hayo yalifanyika kwa faragha, Meya wa Tivaouane, Demba Diop Sy aliliambia shirika la habari la AFP.“Tunaomboleza uchungu walio nao wana familia, aliongeza. Leo ni siku ya mama nchini Senegal, na kuna kina mama 11 ambao wamepoteza watoto wao”.

Hitilafu ya umeme imetajwa kuwa chanzo cha moto huo katika hospitali ya Mame Abdou Aziz Sy Dabakh.