Ukraine, washirika walaani shambulizi katika kituo cha reli, wailaumu Russia

Wanajeshi wa Ukraine wakiwa pembeni ya kipande cha kombora la Tochka-U baada ya tukio la Russia kulipiga katika kituo cha reli huko mjini Kramatorsk, Ukraine, Ijumaa, April 8, 2022. (AP Photo/Andriy Andriyenko)

Ukraine na washirika wake wamelaani shambulizi la kinyama lakombora lililoelekezwa kwenye mkusanyiko wa watu waliokuwa katika kituo cha reli Ijumaa, wakiilamu Russia kwa mauaji hayo.

Maafisa wa reli wa Ukraine wamesema takriban watu 52 wameuwawa, wakiwemo watoto watano, na kiasi cha watu 87 wamejeruhiwa katika kituo hicho kilichopo katika mji wa mashariki mwa Ukraine wa Kramatorsk, uliokuwa unatumika kupitisha raia wanaoondoka nchini.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy ameliita shambulizi hilo ni la makusudi dhidi ya raia.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy (Ukrainian Presidential Press Office via AP)

“Bila ya nguvu na ushujaa wa kusimama kwa ajili yetu katika uwanja wa vita, (wanajeshi wa Russia) wanaendelea kuangamiza makundi ya raia,” Zelenskyy alisema kupitia mitandao ya jamii.

Katika hotuba yake wakati wa usiku kwa njia ya video Ijumaa, Zelenskyy alisema, “ Tunatarajia jibu thabiti la kimataifa dhidi ya uhalifu huu wa kivita.”

Alisema juhudi zitachukuliwa na Ukraine “ kusajili kila dakika kuonyesha nani alifanya nini, nani alitoa amri gani, makombora hayo yalitokea wapi, nani aliyasafirisha, na nani alitoa amri na vipi shambulizi hili liliafikiwa.”

Wizara ya Ulinzi ya Uingereza ilisema katika taarifa zake mpya za ujasusi Jumamosi kuwa Russia inaendelea “kuwashambulia Waukraine ambao siyo wanajeshi, kama wale waliouwawa katika shambulizi la roketi jana katika kituo cha reli.

Rais wa Russia Vladimir Putin (Mikhail Klimentyev, Sputnik, Kremlin Pool Photo via AP)

“Utashi wa Russia ni kuweka njia ya ardhini kati ya Crimea na Donbas,’ na wizara ilisema pia, hilo linashindikana kutokana na upinzani kutoka jeshi la Ukraine.

Zelenskyy, katika mahojiano yaliyopangwa kurushwa hewani katika televisheni ya Marekani Jumapili katika kipindi cha ‘60 minutes’ kupitia kituo cha televisheni cha CBS, alisema Ukraine imewaweka chini ya ulinzi marubani wa Russia ambao walikuwa na ramani zinazoonyesha maeneo ya raia yaliyokuwa yamepangwa kupigwa mabomu.

Rais wa Marekani Joe Biden alisema katika ujumbe wa Twitter kuwa shambulizi hilo ni mauaji mengine ya kinyama yaliyofanywa na Russia,” wakati Waziri wa Ulinzi wa Uingereza Ben Wallace alisema “shambulizi hilo la raia na miundombinu muhimu ni uhalifu wa kivita.”

Rais wa Marekani Joe Biden (AP Photo/Susan Walsh)

Umoja wa Mataifa umetamka kuwa shambulizi hilo la kituo cha reli na mashambulizi mengine “hayakubaliki hata kidogo” na “ni ukiukaji mkubwa wa sheria za kimataifa za kibinadamuna na sheria za kimataifa za haki za binadamu, ambapo wanaotekeleza uhalifu huu lazima wawajibishwe.”

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric amerejea kusisitiza wito wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres wa kusitishwa mara moja ukatili huu wa kivita.”