Katika kikao kilichojaa majibizano na hisia kali, kiongozi wa chama cha Leba Keir Starmer aliwauliza wabunge “kwa nini huyu bado yuko madarakani” Truss, alijibu kwa kusema….
''Bw. Spika, mimi ni mpiganaji. Mimi sio mtu wa kukata tamaa. Hatua ambazo nimechukua ni kwa maslahi ya taifa ili kuhakikisha kwamba tuna hali ya uchumi ambayo ni nzuri."
Truss amehudhuria kikao chake cha kwanza cha kujibu maswali ya wabunge hii leo, tangu alipomteua Jeremy Hunt kuwa waziri wa fedha.
Waziri mkuu ameomba msamaha
Ameomba msamaha kwa bunge na kukiri kwamba alikosea kutokana na mpango wake wa uchumi. Baadhi ya wabunge walikatiza hotuba yake kila mara wakipaza sauti na kumtaka ajiuzulu.
Kiongozi wa chama cha leba Starmer alimshambulia zaidi.
''Bw Spika, mamlaka pekee aliyowahi kuwa nayo kutoka kwa wabunge wa upinzani ilikuwa ya kujenga uchumi, na hilo lilimalizika vibaya sana. Nchi haikupata chochote cha kuonyesha kando na uharibifu wa uchumi. Miaka miwili ya nishati ya bure imekwenda hivyo, mpango wa ununuzi bila kodi umeharibika, na yule ambaye alionekana kuwa rafiki yake mkubwa, aliyekuwa Kansela, naye amekwenda. Wote wamekwenda."