Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Mei 08, 2024 Local time: 15:10

Watu 8 bado wanashikiliwa na polisi Kenya


Polisi wa Kenya na wananchi wengine katika jengo la Westgate huko Nairobi September 21, 2013.
Polisi wa Kenya na wananchi wengine katika jengo la Westgate huko Nairobi September 21, 2013.
Maafisa wa Kenya wanasema bado wanawashikilia watu wanane kuhusiana na shambulizi la siku nne lililosababisha vifo kwenye jengo la maduka ya kifahari mjini Nairobi.

Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Kenya, Joseph Ole Lenku aliwaambia waandishi wa habari Ijumaa kwamba maafisa wamewaachia washukiwa wengine watatu.

Mwanzoni mwa wiki hii maafisa walisema washukiwa wanamgambo watano waliuwawa wakati wanajeshi na polisi walipokuwa wakifanya operesheni ya kukomboa jengo la Westgate. Idadi rasmi ya vifo kutokana na shambulizi hilo imefikia 72.

Wachunguzi wanaendelea kupekua kwenye vifusi vya jengo hilo lililoanguka Ijumaa ya wiki iliyopita. Shirika la msalaba mwekundu nchini Kenya lilisema watu 59 bado hawajulikani walipo kutokana na shambulizi hilo.

Lenku alisema hakuna miili yeyote iliyopatikana kutoka kwenye eneo la tukio. “kwa mujibu wa rekodi za polisi, hakuna ripoti rasmi ya watu waliopotea ambao yawezekana walikuwa kwenye jengo hilo wakati shambulizi likitokea”.

Kundi la wanamgambo wa al-Shabab lenye makao yake nchini Somalia lilidai kuhusika kwa shambulizi na linaapa kufanya mashambulizi zaidi dhidi ya Kenya.

Katika mtandao wa Twitter Ijumaa kundi hilo la wanamgambo lilisema shambulizi lake kwenye jengo la Westgate lilikuwa ni mwanzo wa mashambulizi yanayotarajiwa kufanywa nchini humo.
XS
SM
MD
LG