Uchunguzi mpya uliofanywa na Sauti ya Amerika umebaini hisia mbalimbali za kisiasa miongoni mwa raia wa Somalia, taifa lililogubikwa na vita. Zaidi ya wasomali elfu 3 kote nchini Somalia walishiriki katika uchunguzi juu ya rasimu ya katiba mpya kwa nchi yao.
Zaidi ya robo tatu ya washiriki waliunga mkono rasimu hiyo ya katiba mpya . Wengi wao waliunga mkono kushirikishwa kwa sharia za kiislam. Na waligawanyika katika maoni yao juu ya kushirikisha wanawake katika maswala ya kisiasa, huku wengi wakiunga mkono uhuru wa vyombo vya habari.
Washiriki wengi pia waliunga mkono serikali kuu yenye nguvu katika taifa hilo lililogawanywa na mitafaruku ya kivita na ukosefu wa kanuni za kisheria. Uchunguzi huo wa Sauti ya Amerika ulifanywa kwa msaada wa teknolojia kutoka kwa mtandao wa mawasiliano wa Google.
Nayo idhaa ya Kisomali ya Sauti ya Amerika ilipokea zaidi ya simu elfu 20 katika uchunguzi huo na kuwapeleka waandishi habari wake katika maeneo yasiyofikika kwa urahisi ya Somalia kufanya mahojiano na wananchi. Mkuu wa idhaa hiyo Abdirahman Yabarow, alisema maeneo yanayodhibitiwa na wanamgambo wa al-Shabab yalikuwa magumu zaidi kuweza kufanya uchunguzi huo.