Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Mei 08, 2024 Local time: 04:02

Wanasayansi wa hali ya hewa wasema wiki za karibuni zimekuwa na joto zaidi ulimwenguni


Msichana akijimiminia maji usoni na kichwani mbele ya kanisa lililo katikati ya jiji la Messina, kwenye kisiwa cha Sicily, wakati wa wimbi la joto Julai 16, 2023. (AFP)
Msichana akijimiminia maji usoni na kichwani mbele ya kanisa lililo katikati ya jiji la Messina, kwenye kisiwa cha Sicily, wakati wa wimbi la joto Julai 16, 2023. (AFP)

Wanasayansi wa hali ya hewa wasema wiki za karibuni zimekuwa na joto zaidi ulimwenguni na huenda ndizo zenye joto la juu zaidi katika miaka 100,000 iliyopita

Baadhi ya sehemu hivi sasa zimeingia chini ya maji na nyingine kwenye joto kali lakini kwa watalii wa fukwe za Bahari, athari za mabadiliko ya hali ya hewa inatishia uwepo wao na mtindo wa maisha yao.

Moto mkali uliteketeza misitu na nyumba kwenye kisiwa cha Uhispania cha La Plama huku upepo ukichochea moto huo. Mamlaka za huko zinasema zaidi ya watu elfu nne wamehamishwa huku Ulaya ikikabiliwa na wimbi la joto.

Takriban watu elfu 61 huenda wamefariki dunia kwa joto kali barani humo msimu uliopita wa kiangazi kulingana na makadirio ya hivi karibuni yaliyochapishwa kwenye jarida la Nature.

Katika mji mkuu wa India, mvua kubwa ilizamisha barabara chini ya maji. New Delhi iko katika msimu wake wa kawaida wa Monsoon lakini imeshuhudia mvua isiyo ya kawaida karibu mara 10 ya inavyotarajiwa kwa wakati huu wa mwaka.

Kaskazini-mashariki mwa Marekani, mvua kubwa zilisomba barabara, na watu kulazimika kuhama, na kuzuia ndege kuruka. Dhoruba hizo zilipiga sehemu za New England, New York, na Connecticut huku baadhi ya maeneo yakiripoti mvua zaidi ya sentimeta 10.

Ni kutokana na hali hii kwamba tunaingia chini ya maji kwenye ufuo wa Florida, ambapo wanasayansi wanasema hali ya joto kali inapelekea uharibifu kwenye miamba ya matumbawe na mfumo mzima wa ikolojia wa baharini.

"Mbali na kuwa na hali ya joto ya juu sana ardhini, pia tuna joto la juu sana la bahari. Na kwa hivyo baadhi ya tovuti za ufuatiliaji wa muda mrefu hapa Miami zinaanza kuonyesha dalili za upaukaji wa mapema wa matumbawe. Kwa hivyo, zinaanza kupauka na kupoteza matumbawe yao, rangi zao za mwani na hatimaye tunatarajia zitapauka kabisa" alisema Michael Sulivan kutoka Chuo kikuu cha Miami anasema

Mamlaka ya Kitaifa wa Bahari na Anga, au NOAA, inaelezea upaukaji wa matumbawe kama matumbawe yakiondoa mwani wake kutokana na mambo mengine kama vile mabadiliko ya joto la maji. NOAA inasema mwaka wa 2005, Marekani ilipoteza nusu ya miamba ya Caribbean katika mwaka mmoja kutokana na kupauka. Lakini wanasayansi wanaofanya kazi katika mradi wa kurejesha miamba hiyo wanasema wanaona dalili za matumaini katika sehemu isiyotarajiwa kando ya maeneo ya maji ambapo meli kubwa za kusafiri hujipanga.

"Tuko ndani kabisa ya bandari hivi sasa, na kwa ujumla kuna machafuko makubwa maji ya moto hukaa hapa kwa muda mrefu. Kwa hivyo siyo kile tunachofikiria kuwa makazi ya kawaida ya miamba ya matumbawe. Lakini kando ya ufuo huu ulioimarishwa kuna mawe makubwa, tuna matumbawe ambayo yametulia na yanastawi. Haya ni baadhi ya matumbawe yenye afya zaidi ambayo nimewahi kuona kote Miami na yanakuwa makubwa sana na yanaonekana kuwa na afya" aliongeza Sullivan.

Wanasayansi wanasema mbinu hii mpya ya kuzalisha na kupandikiza matumbawe yenye afya inaweza kuwa njia ya kusaidia kuwepo kwao, kabla ya ya kuyaingiza tena baharini . Wataalam wanasema miamba ya matumbawe hutengeneza makazi ya mamilioni ya viumbe na kuongeza utando wa chakula cha baharini wenye afya na kulinda ukanda wa pwani .Pia ni kivutio cha watalii ambacho kinasaidia uchumi wa ndani wa jimbo la Florida.

Forum

XS
SM
MD
LG