Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 22:30

Msumbiji Kaskazini yakabiliwa na mzozo wa kibinadamu


Watu waliokimbia Palma kutokana na mashambulizi ya wanamgambo wa Kiislam wamekusanyika ili kupata msaada huko Pemba, Msumbiji, April 2, 2021.
Watu waliokimbia Palma kutokana na mashambulizi ya wanamgambo wa Kiislam wamekusanyika ili kupata msaada huko Pemba, Msumbiji, April 2, 2021.

Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanaonya kwamba eneo la Kaskazini mwa Msumbiji linakabiliwa na mzozo wa kibinadamu na usalama kwa muda mrefu kutokana na mizozo, njaa na magonjwa ambayo yamewakabili maelfu ya watu katika eneo hilo.

Watu bado wanakimbia katika makundi kutokana na athari za vurugu zilizozuka kaskazini mwa mji wa pwani wa Msumbiji wa Palma. Wengi wa maelfu ya watu ambao wamekimbilia Pemba, mji mkuu wa Cabo Delgado, wanasimulia habari za mashambulizi ya kutisha yaliyofanywa na wanamgambo wa Kiislamu, ambao waliripotiwa kuuwa dazeni ya watu na kufanya ukatili mwingine.

Akizungumza kwa njia ya video kutoka Pemba, mkurugenzi wa dharura wa mfuko wa watoto wa Umoja wa Mataifa Manuel Fontaine anasema watu wanaeleza namna walivyolazimika kukimbia katikati ya usiku. Wanazungumza kwa huzuni juu ya familia kutenganishwa wakati wakiokoa maisha yao.

UNICEF inasema viwango vya utapiamlo kati ya watoto waliokimbia makazi yao huko Cabo Delgado ni juu sana, na takriban 33,000 wanahitaji lishe maalum ya kuokoa maisha. Inasema kipindupindu na COVID-19 vinatia wasiwasi.

Shirika hilo limetoa wito wa dola milioni 52.8 kwa Msumbiji mwaka huu, dola milioni 30 za kiasi hicho kinatakiwa kwenda Cabo Delgado. Inasema asilimia 37 tu ya maombi hayo yanafadhiliwa na msaada wa kimataifa kwa operesheni yake ya kibinadamu ambayo inahitajika haraka.

Katika ombi jingine tofauti, Mpango wa Chakula Ulimwenguni unaomba dola milioni 82 ili kuongeza msaada wa chakula kaskazini mwa Msumbiji. Msemaji wa WFP, Tomson Phiri amesema kufuatia mashambulizi mabaya huko Palma, familia na watu binafsi wamelazimika kuacha nyumba zao, mali zao na maisha ili kukimbilia kwenye usalama.

Phiri anasema WFP imepanga kusaidia wakimbizi wa ndani 750,000 na watu walio katika mazingira magumu wa jamii zinazowapokea huko Cabo Delgado na majimbo mengine matatu ya kaskazini. Amesema WFP inandaa usambazaji wa dharura wa chakula kwa familia ambazo zimekimbia ghasia huko Palma.

XS
SM
MD
LG