Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 11:39

Wanadiplomasia Saudia wadadisi vita vya ufisadi


Picha zinazo waonyesha Mfalme wa Saudi Arabia Salman bin Abdulaziz Al Saud na Mrithi wa Ufalme Mohammed bin Salman, huko Riyadh, Saudi Arabia, Nov. 9, 2017.
Picha zinazo waonyesha Mfalme wa Saudi Arabia Salman bin Abdulaziz Al Saud na Mrithi wa Ufalme Mohammed bin Salman, huko Riyadh, Saudi Arabia, Nov. 9, 2017.

Wiki moja baada ya zoezi la kukamatwa kwa baadhi ya wana wa mfalme wa Saudi Arabia kitendo ambacho hakijawahi kutokea katika historia ya nchi hiyo, wadadisi wa kidiplomasia wanashuku iwapo hii ni vita ya ufisadi peke yake.

Serikali mbalimbali duniani na wawekezaji bado wanajaribu kujibu maswali ya msingi juu ya zoezi hilo la kamatakamata ambalo serikali ya Saudi Arabia inaeleza kuwa ni vita dhidi ya ufisadi inayoendeshwa na aliyeteuliwa kuwa mrithi wa mfalme wa nchi hiyo.

Swali liliopo hivi sasa ni iwapo Mohammad bin Salman mwenye umri wa miaka 32 ameanza kujiandaa kuchukua madaraka ili kuhakikisha kuwa urithi wake hautokabiliwa na matatizo wakati baba yake ambaye ni mgonjwa atakapokufa?

Au yeye ni kama vile anavyojielezea, ni mwanamabadiliko aliyedhamiria kuibadilisha falme hiyo kutokana na misimamo mikali ya kiutawala ambayo ilikuwa inashinikizwa na vitengo mbalimbali vya familia hiyo pana ya kifalme.

Habari zilizoenea ambazo hazikuthibitishwa katika mji mkuu wa Saudia zinaeleza kuwa kamatakamata hiyo iliyohusisha matajiri wakubwa na wafanyabiashara inaonekana kuwa haijamalizika na huenda kukawa na watu zaidi watakao kamatwa kama ilivyotabiriwa na wanadiplomasia wakigeni walioko nchini Saudi. Wanadiplomasia hao wameshtushwa na ukamataji huo.

Hata hivyo vijana wa kipato cha kati Saudia, ambao wamekatishwa tamaa na kuwepo rushwa na mtizamo finyu ya utawala huo wa kifalme, wanashangilia kitendo cha mrithi wa ufalme kuendesha operesheni hiyo.

Kwa upande wao wawekezaji wanachukua tahadhari , wakihofia kuwa Mohammad bin Salman ameuma kile ambacho hawezi kukitafuna.

Kwa muda mrefu ikiangaliwa kama ni sehemu yenye utulivu kufanya biashara, hatua za kutumia nguvu zilizojitokeza zimeshuhudia takriban watu 500 wakikamatwa, akiwemo mtu tajiri kuliko wote nchini humo, Mwana wa mfalme Waleed bin Talal.

Talal ni bilionea mfanyabiashara ambaye ni mshirika wa umiliki wa hoteli za Four Sessions na hivi karibuni alikuwa mwekezaji mkuu wa himaya ya vyombo vya habari ulimwenguni ya Rupert Murdoch. Alikamatwa akiwa katika kambi yake ya kifahari iliyoko jangwani.

Viongozi wa kijeshi maarufu pia walikumbwa na wimbi hilo la ukamataji, akiwemo mwana wa mfalme Miteb bin Abdullah, waziri wa jeshi maalum la askari 100,000 ambaye ni mtoto wa marehemu Mfalme Abdullah, ambaye kifo chake miaka miwili iliyopita kilipelekea Mohammed bin Salman kuchaguliwa kuwa mrithi wa mfalme na mtawala wa hivi sasa mwenye umri wa miaka 81.

XS
SM
MD
LG