Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:44

Walionusurika na mauaji ya Rwanda walaani makala ya BBC


Picha za mafuvu katika maadhimisho ya miaka 20 ya mauaji ya halaiki nchini Rwanda
Picha za mafuvu katika maadhimisho ya miaka 20 ya mauaji ya halaiki nchini Rwanda

Watu walionusurika na mauaji ya halaiki nchini Rwanda wamelaani makala maalum iliyoandaliwa na kurushwa na kituo cha television cha BBC II kuhusu mauaji ya Rwanda. Mwandishi wa makala hayo alieleza kwamba kuanguka kwa ndege ya rais wa zamani nchini Rwanda mwaka 1994 ilikuwa sababu ya kutokea mauaji ya halaiki nchini humo suala ambalo linakanushwa vikali na serikali ya Rwanda na walionusurika na mauaji hayo.

Makala hiyo iliyopewa jina “The untold story about Rwanda” ikiwa na maana hadithi isiyotajwa kuhusu Rwanda. Mwandishi wake Jane Corbin ambaye pia ni mwandishi wa habari wa kituo cha televisheni cha BBC alikwenda Rwanda mwezi April mwaka huu wakati wa kumbukumbu ya mauaji ya Rwanda ya mwaka 1994. Makala haya yanafafanua jinsi ya mauaji ya Rwanda yalivyoanza na kufanayika.

Lakini walionusurika na tukio hilo pamoja na serikali kwa jumla wanaona kile kilichoko kwenye makala hiyo ni upotoshaji wa ukweli wenyewe na kupinga kabisa kutokea kwa mauaji ya Rwanda.

katika tangazo lililotolewa kwa vyombo vya habari na jumuiya ya kutetea haki za walionusurika na mauaji hayo IBUKA limelitaka shirika la habari la BBC kuacha kabisa kutangaza makala hiyo lakini zaidi kutathmini mienendo ya baadhi ya wafanyakazi wake.

Tangazo hilo linasema kwamba ukweli kwamba mwandishi huyo alikwenda Rwanda mwaka huu na kushindwa kuzungumza na walionusurika na mauaji hayo na badala yake akaamua kuzungumza na wapinzania wa serikali ya Rwanda ambao wengi wao walikuwa na mkono kwenye mauaji hayo ni ishara tosha kwamba mwandishi huyo Jane Corbin alikuwa na agenda ya siri.

Mwanasheria wa kimataifa ambaye pia ni mmoja wa walionusurika na mauaji hayo Dr. Bideri Justin anasema sakata hii inaweza kuleta athari.

“Ni uamuzi wa hatari kabisa ambao unapotosha historia ya nchi ya Rwanda lakini kubwa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994. Watu wanaofanya hivi kwa kiasi kikubwa huwa na maslahi binafsi”.

Katika hatua iliyowakasirisha wengi walionusurika ni pale mwandishi huyo anapotaja kwamba nchini Rwanda walifariki watu 200,000 tofauti na idadi inayotajwa na Rwanda ya wahanga milioni moja au ile iliyoidhinishwa na Umoja wa Mataifa ya watu 800,000.

Vile watu aliowahoji kwenye makala hiyo wengi wao wanatajwa kuwa wapinzani wa serikali ya Rwanda wanaoishi uhamishoni.

Jumuiya inayotetea haki za walionusurika na mauaji hayo inasema inashangazwa na mwandishi huyo kuamua kuwahoji watu hao na kushindwa kuwapa nafasi wale walionusurika suala ambalo wanasema ni kukiuka maadili ya uandishi wa habari ya kutolalia upande wowote.

Hata hivyo mwanasheria Bideri Justin anasema ukweli unabaki pale pale. “Wengi wanafahamu fika kilichotokea Rwanda, kundi la watu wachache linalojaribu kupotosha ulimwengu linaweza kuwa hatari lakini ni jukumu la watu wote kuhakikisha ukweli unabakia bila chembe ya uongo”.

Aidha Makala hiyo inasemaa kwamba kuanguka kwa ndege ya rais wa zamani wa Rwanda ilikuwa chanzo cha mauaji hayo ya halaiki kitu ambacho hakipatiwi uzito na serikali pamoja na walionusurika wakisema kwamba hata kabla ya kutunguliwa ndege hiyo mauaji hayo dhidi ya kabila la watutsi yalianza zamani.

Haijulikani sakata hii itaishia wapi lakini mwaka 2008 Rwanda iliwahi kufunga matangazo ya Idhaa ya BBC katika lugha ya kinyarwanda kutokana na shutuma za kutoa nafasi kwa wapinzani na kutokea kwa mauaji hayo na kueneza itikadi ya ubaguzi. Lakini baadaye hali ilirudi kuwa ya kawaida.

XS
SM
MD
LG