Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 00:11

Vyombo vya habari vya Qatar  vyajibu ukosoaji wa Ulaya


Picha ya Neymar Jr wa Brazil inaonekana kwenye jengo moja huko Doha Qatar REUTERS/Hamad I Mohammed
Picha ya Neymar Jr wa Brazil inaonekana kwenye jengo moja huko Doha Qatar REUTERS/Hamad I Mohammed

Vyombo vya habari vya Qatar vinavyodhibitiwa vikali hivi karibuni vilijibu ukosoaji wa Ulaya dhidi ya rekodi ya haki za binadamu ya nchi hiyo ya Ghuba kabla ya Kombe la Dunia, ambalo nchi hiyo imetumia mabilioni ya dola kuandaa.

Magazeti ya Ulaya na makundi ya kutetea haki za binadamu yameweka bayana rekodi ya Qatar kuhusu wafanyakazi wahamiaji, wanawake na jamii ya wapenzi wa jinsia moja katika maandalizi ya michuano hiyo itakayoanza Novemba 20 na inatarajiwa kuvutia mashabiki zaidi ya milioni moja.

Baadhi ya miji ya Ufaransa imesema haitaruhusu TV za umma kuwekwa ili kuonyesha mechi katika kupinga ukiukaji wa haki.

Gazeti la Al Sharq lilionyesha kwa ufasaha katuni yenye Kombe la Dunia iliyozingirwa na mishale inayoashiria ukosoaji ambao Qatar imekabiliana nao.

Tahariri katika gazeti la Al Raya ilisema magazeti ya Ulaya yamekuwa yakiendelea na mashambulizi yao kwenye Kombe la Dunia nchini Qatar tangu ilipotangazwa Desemba mwaka 2010.

“Msirudie makosa ya zamani," ilionya, ikiangazia ripoti ya Washington Post ya mwaka 2015 kuhusu idadi ya wafanyakazi wahamiaji waliouawa kwenye miradi ya Kombe la Dunia ambayo ilirekebishwa baada ya maandamano ya kuipinga serikali ya Qatar.

"Hebu tuache kampeni za kupaka matope na tushirikiane kwa ajili ya Kombe la Dunia ambalo linaunganisha watu," iliongeza.

Al Sharq ilifanya mahojiano na Lakhdar Belloumi, mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Algeria anayechukuliwa kuwa mmoja wa wachezaji bora wa kandanda wa Kiarabu wa wakati wote, ambaye alisema kampeni zenye nia mbaya hazitaikatisha tamaa Qatar.

Tahariri katika gazeti la Jumapili ilikashifu "uongo, uvumi na kashfa" zilizoandikwa Ulaya kuhusu maandalizi ya Kombe la Dunia la Qatar.

Ilisema kulikuwa na "njama ya kimfumo" na vyombo vya habari katika nchi nyingi za Ulaya juu ya habari kuhusu haki za wafanyakazi nchini Qatar, "wakati vyombo vya habari hivyo vimesahau mazingira mabaya ya kazi wanayokumbana nayo wafanyakazi huko Ulaya.

“Tunagundua kuwa vyombo vya habari hivi vyenye shida vinatengeneza hadithi kila wakati nchi kutoka nje ya bara hilo linapoandaa mashindano," alisema Al Sharq.

Katika makala kwenye gazeti la lugha ya Kiingereza la Doha News, msanii Ghada Al Khater aliandika: "Nisamehe kwa kutilia shaka nia kama hiyo ya nchi za Ulaya, ambazo kwa muongo mmoja uliopita zimesimama na kutazama wahamiaji wanaokimbia migogoro, uharibifu na umaskini wakizama hadi chini ya Mediterania”.

Amiri wa Qatar Sheikh Tamim bin Hamad Al-Thani alilalamika mwaka huu kuhusu mashambulizi dhidi ya mataifa ya Kiarabu lakini aliliambia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwezi uliopita kwamba mashabiki wote watakaribishwa kwenye Kombe la Dunia "bila ubaguzi."

XS
SM
MD
LG