Wawaniaji wa urais wa Marekani Hillary Clinton na Donald Trump ambao wanatafuta tikiti za kuwakilisha vyama vyao vya kisiasa kwenye uchaguzi utakaofanyika mwezi Novemba, waliibuka washindi katika uchaguzi wa awali uliofanyika Jumamosi kwenye majimbo mawili ya Nevada na South Carolina mtawalia.
Bi Clinton alimshinda mpinzani wa pekee katika chama cha Democratic, Seneta Bernie Sanders, kwa kupata asili mia 52.6 ya kura zote zilizopigwa huku Bw Sanders akipata asili mia 47.3 kwenye kura hiyo ya awali katika jimbo la Magharibi mwa Marekani la Nevada.
Bwana Trump, ambaye ni mfanya biashara bilionea aliyegeuka mwanasiasa alizoa asili mia 34 ya kura za South Carolina na kuwashinda wapinzani wake wa karibu, Seneta wa Florida Marco Rubio na mwenzake wa Texas Ted Cruz kwa Zaidi ya asili mia kumi.
Wakati wa hotuba yake Bi Clinton alishangiliwa kwa vifijo na nderemo aliposema kuwa hajawahi kuwa na shaka kuhusu uungwaji mkono na wapiga kura wa jimbo la Nevada na kwamba alijua angepata matokeo mema.
Trump naye aliwaambia wafuasi wake kwamba hakuna jambo rahisi katika uwaniaji wa urais nchini Marekani. “Ni kazi ngumu sana, lakini mtu anafurahi sana anaposhinda,” alisema Trump aliyeandamana na familia yake yote kwenye jukwaa.
Bwana Trump ambaye awali mwezi huu alipata ushindi katika jimbo la New Hampshire ambao uliinua nafasi yaka baada ya kushindwa na Ted Cruz katika uchaguzi wa jimbo la Iowa, alionekana mwenye furaha huku akikariri kauli mbiu yake ya "Tutauifanya Marekani kuwa taifa lenye nguvu tena" mara kadhaa.
Aliyekuwa gavana wa zamani wa Florida, Jeb Bush, ambaye ni kakaye rais wa zamani wa Marekani George W. Bush na mwanaye rais mwingine wa zamani George H W Bush, alitangaza kujiondoa kutoka kwa kinyang'anyiro hicho Jumamosi usiku, baada ya kushindwa vibaya katika majimbo matatau yaliyopiga kura ya awali.
Sasa uwanja wa Warepublican umesalia na wawaniaji tano - walipoanza walikuwa 17 - ambao wanajiandaa kwa uchaguzi wa awali kwenye jimbo la Nevada siku ya Jumanne huku Wademokrat wakiwa na wawaniaji wawili watakaoshiriki kwa uchaguzi wa awali kwenye jimbo la South Carolina siku siku ya Jumamosi tarehe 27 mwezi huu.