Ujerumani inapanga kuimarisha sheria zake za umiliki wa silaha kufuatia njama inayoshukiwa kufanywa na kundi la siasa kali za mrengo wa kulia kutaka kuipindua serikali na kuuweka ufalme mdogo kama kiongozi wa kitaifa, waziri wake wa mambo ya ndani amesema katika mahojiano yaliyochapishwa jumapili.
Polisi wa Ujerumani wiki iliyopita waliwakamata watu 25 wanaoshukiwa kuhusika na njama hiyo, jambo ambalo limewashtua wengi katika moja ya demokrasia thabiti barani Ulaya. Wengi wa washukiwa walikuwa wanachama wa vuguvugu la siasa kali za mrengo wa kulia la "Reichsbuerger" (Raia wa Reich) kundi ambalo linakanusha kuwepo kwa taifa la kisasa la Ujerumani kulingana na waendesha mashtaka.
Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Ujerumani Nancy Faeser, katika mahojiano na gazeti la "Bild am Sonntag", alionya kuwa kundi la Reichsbuerger (Raia wa Reich) linawakilisha kitisho kinachoongezeka kwa Ujerumani ikizingatiwa kuwa limepanuka kwa watu 2,000 hadi 23,000 katika mwaka uliopita.
Wakati huo huo waendesha mashtaka wamesema washukiwa hao ni pamoja na watu wenye silaha na ujuzi wa jinsi ya kuzitumia. Walikuwa wamejaribu kuajiri wanajeshi wa sasa na wa zamani na walikuwa wamehifadhi silaha.