Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 11:51

Uhuru: Wanasiasa wamefanya watu wa jamii yangu wanichukie bila sababu


Rais wa Kenyatta Uhuru Kenyatta. PICHA: AFP
Rais wa Kenyatta Uhuru Kenyatta. PICHA: AFP

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta amesema kwamba watu kutoka mlima Kenya, wamehadaiwa na wanasiasa na kuwafanya kumchukia bila sababu yoyote.

Bila kutaja jina la mtu yeyote, Kenyatta amesema kwamba anasikitika kuwa watu wa jamii yake kwa jumla walihadaiwa na baadhi ya wanasiasa na kumchukia, kiasi cha kutotaka kumsikiliza.

“Watu wangu katika mlima Kenya wamehadaiwa na kuamini kwamba mpango wangu wa mamlaka kuwa mikononi mwa mtu mmoja anayeshinda uchaguzi ni mbaya. Lakini sasa, nitakuwa nikicheza na wajukuu zangu huku shida za Kenya zikiendelea kuwepo,” Uhuru amesema wakati wa kikao na waandishi wa habari kutoka mlima Kenya.

Kikao hicho kwa lugha ya Kikuyu, kilipeperushwa na vyombo vyote vya habari vinavyoeperusha matangazo katika lugha hiyo.

Amesema kwamba “kutokana na ujinga wao, hawezi kuwasaidia,” na kwamba wakati wa utawala wake, amekuwa akiweka maslahi ya taifa mbele ya maslahi yake binafsi.

Kura za maoni zinaonyesha Ruto ana ufuasi mkubwa mlima Kenya

Ukusanyaji wa maoni unaonyesha kwamba naibu rais William Ruto ana ufuasi mkubwa katika mlima Kenya – Jamii ya Kikuyu – yake Uhuru Kenyatta, licha ya Kenyatta kutaka watu wa jamii yake kumuunga mkono Raila Odinga.

Kenyatta alimteua wakili wa muda mrefu, aliyekuwa waziri wa sheria Martha Karua kuwa mgombea mwenza wa Raila Odinga ili kuwashawishi wakaazi wa sehemu hiyo kumuunga mkono Raila Odinga lakini ukusanyaji maoni ambao umefanywa na kampuni mbalimbali unaonyesha kwamba hakuna mabadiliko yametokea.

William Ruto alimteua Rigathi Gachagua kuwa mgombea mwenza. Gachagua vile vile anatoka Mlima Kenya.

Kulingana na tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC, maeneo ya mlima Kenya – jamii ya Uhuru Kenyatta – na Rift Valley – jamii ya William Ruto – ndiyo yanaongoza kwa idadi kubwa ya wapiga kura kote Kenya.

Rifty Valley lina jumla ya wapiga kura milioni 5.3 huku mlima Kenya likiwa na wapiga kura milioni 5.7.

Changamoto kubwa zilizomkumbana Uhuru akiwa madarakani

Rais Uhuru Kenyatta amesema kwamba ukabila ni mojawapo ya changamoto kubwa ambazo amekumbana nazo akiwa madarakani. Amesema kwamba amejaribu kuiunganisha nchi hiyo bila kuzingatia ukabila lakini hajafanikiwa na kwamba anatumai kwamba kiongozi atakayeingia madarakani baada yake atafanikiwa.

Anaamini kwamba jaribio la kubadilisha katiba lililofeli maarufu kama BBI lingesaidia kumaliza ukabila.

XS
SM
MD
LG