Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 09:36

Siku ya upigaji kura Marekani


Watu wakiwa katika msitari wa kupiga kura Arlington, Virginia
Watu wakiwa katika msitari wa kupiga kura Arlington, Virginia

Wamarekani wanapiga kura katika uchaguzi wa katikati ya awamu leo ambao utaamua endapo chama cha Republican cha Rais Donald trump kitaendelea kudhibiti mabaraza yote mawili ya bunge la marekani – Congress - au wademokrat watapata udhibiti ingawa wa baraza moja la bunge hilo.

Viti vyote 435 katika baraza la wawakilishi vinagombaniwa katika uchaguzi huu, pamoja na viti 35 kati ya 100 kwenye baraza la seneti, na vilevile nafasi za ugavana katika majimbo 50. Uchaguzi huu pia unachukuliwa kama kura ya maoni kuhusu utawala wa Rais Donald Trump.

Jengo la Bunge la Marekani, Capitol
Jengo la Bunge la Marekani, Capitol

Utafiti wa maoni ya watu unaonyesha kuwa wademokrat wana nafasi nzuri ya kuchukua udhibiti wa baraza la wawakilishi, wakiwa wanahitaji kupata viti 23 zaidi kuwa na wingi katika baraza hilo. Warepublican wanatumanini kuwa juhudi za kampeni za Rais Trump zimewashawishi wafuasi wao vya kutosha ili waendelee kushikilia udhibiti wa viti 51 kwa 49 walio nao katika baraza la seneti.

Kwa kiasi kikubwa inategemea watu wangapi watajitokeza kupiga kura leo. Katika historia ya Marekani Warepublican mara nyingi wanajitokeza zaidi katika uchaguzi wa katikati ya awamu. Hata hivyo, mwaka huu Wademokrat wamefanya juhudi kubwa kuwashawishi wafuasi wao kujitokeza ikiwa ni pamoja na rais wa zamani Barack Obama kujitokeza katika majimbo kadha kuwapigia kampeni wagombea wademokrat.

Historia

Uchaguzi huu pia unatazamiwa kuweka historia Marekani kwa kuingiza mwanamke au wanawake wa kwanza waislamu katika bunge la Marekani. Ilhan Omar, mkimbizi mhamiaji mwenye asili ya kisomali, anagombania kuingia bungeni kutoka Minnesota, na Rashida Tlaib, mzaliwa wa Marekani mwenye asili ya Pakistan, anagombania kuingia bungeni kutokea jimbo la Michigan.

Mgombea ubunge Ilhan Omar
Mgombea ubunge Ilhan Omar

Katika jimbo la Georgia Mdemokrat Stacey Adams anawania kuwa mwanamke wa kwanza Mmarekani mweusi kuwa gavana wa jimbo hilo akipambana vikali na Mrepublican Brian Kemp. Katika wiki za hivi karibuni Adams alipata nguvu mpya baada ya rais wa zamani Barack Obama na mtangazaji maarufu wa televisheni Oprah Winfrey kujitokeza katika jimbo hilo kumpigia kampeni.

XS
SM
MD
LG