Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:07

Trump aanzisha shambulizi jipya dhidi ya uchunguzi maalum


Rais Donald Trump
Rais Donald Trump

Nje ya White House siku ya Ijumaa waandishi walikuwa wamejawa na hasira. Na aliyekuwa amekasirikiwa, ni Rais Donald Trump.

“Mnaweza kuuliza swali moja moja kwa wakati? Ngojea! Swali moja kwa wakati,” Rais aliwakaripia waandishi.

Trump alianzisha shambulizi jipya juu ya uchunguzi unaofanywa dhidi ya Russia wakati tayari kuna ripoti inayokosoa vikali uchunguzi wa barua pepe za Hillary Clinton uliofanywa na mkaguzi mkuu wa Idara ya Sheria.

“Mimi sikufanya kosa lolote. Hapakuwa na hujma yoyote. Hapakuwa na kizuizi chochote sheria kuchukua mkondo wake,” alisema Trump.

"Nayo ripoti ya Mkaguzi Mkuu iliyotoka Jumamosi imekwenda mbali zaidi kuonyesha kuwa, na nafikiri uchunguzi unaofanywa na Mueller kwa jumla umeumbuliwa kabisa."

Lakini ripoti hiyo ilijikita tu katika kuangalia namna Idara ya Uchunguzi wa Makosa ya Jinai ilivyofuatilia barua pepe za Clinton zenye utata.

Pia ilimkosoa mtu ambaye alifukuzwa kazi na Trump akitumikia nafasi ya ukurugenzi wa FBI, James Comey, lakini ilitupilia mbali ile dhana kuwa kulikuwapo juhudi za kisiasa zilizo kuwa zikimlenga Trump.

“Ripoti hii haikupata ushahidi wowote wa upendeleo wa kisiasa au uonevu wowote ambao ulipelekea kuathiri uchunguzi huo ambao unapitiwa tena,” alitangaza Mkurugenzi wa FBI wa hivi sasa Christopher Wray.

Wademokrati pia walitoa maoni yao kuhusu ripoti hiyo.

“Yeyote ambaye anamatarajio ya kutumia ripoto hii kuyumbisha uchunguzi unaofanywa na Mueller au kuthibitisha kuwepo kwa hila ‘iliyobobea ya kitaifa’ dhidi ya Rais Trump bila shaka ataumbuka,” Kiongozi wa chama cha Demokrat katika Baraza la Seneti Chuck Schumer amesema.

Wakati wa kukabiliana na maswali ya waandishi yaliyomchukuwa muda mrefu Ijumaa, Trump pia alitetea mkutano wake hivi karibuni alioufanya na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un.

“Wanachukuwa hatua kukidhi mambo mengi tunayoyataka, na hivi sasa tuko njiani kufikia kuondoshwa kwa silaha za nyuklia,” amesema.

“Na makubaliano yetu yanaeleza kuwa silaha za nyuklia zitaondoshwa kabisa. Hakuna anayetaka kuripoti hilo. Niliweza kushirikiana naye vizuri. Tunasikilizana vizuri. Hili ni jambo zuri, sio kitu kibaya."

Trump pia alikikosoa Chama cha upinzani cha Demokrat na alijaribu kuwatupia lawama kwa hatua za hivi karibuni zilizochukuliwa na utawala wake kuwatenganisha wanafamilia walio kamatwa wakijaribu kuvuka mpaka wa Marekani.

“Wademokrat ndiyo waliolazimisha sheria hiyo katika taifa letu. Nina ichukia sheria hiyo. Nachukia kuona watoto na wazazi wao wakitenganishwa,” Trump alisema.

Baadhi ya Wademokrat katika Bunge la Marekani walimshambulia Rais kwa maoni yake hayo, akiwemo Mbunge mwanamke Michelle Lujan Grisham wa New Mexico.

XS
SM
MD
LG