Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 00:59

Tabang Deng Gai, anasema wamejitolea kurejesha amani kwa wananchi wao


Makamu rais mpya wa Sudan Kusini Taban Deng Gai akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Agosti 17, 2016 huko Nairobi, Kenya.
Makamu rais mpya wa Sudan Kusini Taban Deng Gai akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Agosti 17, 2016 huko Nairobi, Kenya.

Makamu rais mpya wa Sudan Kusini Tabang Deng Gai amesisitiza kuwa nchi yake ina amani na usalama na wanasonga mbele na mageuzi baada ya mapigano katika mji mkuu yaliouwa watu wapatao 300 mwezi uliopita.

Deng alizungumza na waandishi wa habari jijini Nairobi Jumatano alipokuwa nchini humo kukutana na rais Uhuru Kenyatta. Aliwashutumu waandishi wa habari kwa kuripoti taarifa za uongo kwamba mapigano bado yanaendelea Juba na maeneo mengine.

Baada ya kuidhinishwa kwa mapendekezo ya mkutano wa maafisa wa ulinzi wa Afrika Mashariki pamoja na kuidhinishwa kupelekwa kwa majeshi ziada ya kigeni wapatao 4,000 nchini Sudan Kusini, IGAD iliitaka serikali ya Rais Kiir kutekeleza makubaliano hayo kwa njia ya haraka ili kurejesha usalama katika nchi hiyo changa ambayo imekuwa ikikumbwa na msukosuko na vurugu za kisiasa tangu uhuru wake mwaka 2011.

Makamu wa Kwanza wa Rais kuchukua nafasi ya Riek Machar, Taban Deng Gai, anasema kuwa serikali ya Salva Kiir imejitolea kurejesha amani kwa wananchi wake kama njia mojawapo ya kusuluhisha mgogoro na mkwamo wa kisiasa ambao umekuwa ukishuhudiwa nchini humo.

Bwana Gai baada ya kukutana na Rais Kenyatta kumwelezea hatua nchi hiyo imepiga kurejesha utulivu Juba, anasema kuwa majeshi ya Serikali na yale ya Upinzani yataungana hivi karibuni.

Bwana Gai pia anamlaumu aliyekuwa Makamu wa Kwanza Rais Riek Machar kwa kutojitolea kutekeleza mapendekezo ya mkataba wa amani yaliyoafikiwa Addis Ababa kando na kuendesha serikali sambamba kabla ya kugura Juba.

Hata hivyo, afisa mkuu katika kitengo cha Kisiasa katika Kambi ya Riek Machar, Manaseh Zindo,anasema Taban Deng Gai yuko afisini kinyume na sheria. Manaseh Zindo ambaye amekuwa mbunge mteule katika bunge la Kitaifa anasema Makamu huyo wa Kwanza wa Rais, hatambuliki katika mkataba wa amani ulioafikiwa Addis Ababa.

Manaseh Zindo pia anailaumu serikali ya Kiir kwa kuihadaa jamii ya kimataifa kuwa imejitolea kusuluhisha mkwamo wa kisiasa nchini Sudan Kusini.

XS
SM
MD
LG