Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 07:59

Picha kamili ya uvunjifu wa amani ya mshambuliaji wa London


Hoteli ya Preston Park Hotel huko Brighton ambako Khalid Masood alikuwa amelala usiku kabla ya kufanya shambulizi
Hoteli ya Preston Park Hotel huko Brighton ambako Khalid Masood alikuwa amelala usiku kabla ya kufanya shambulizi

Mambo mengi yamejitokeza hivi sasa kuhusu mtu mwenye umri wa miaka 52 ambae aliwaua watu wanne Jumatano na kuwajeruhi dazeni wengine katika Daraja la Westminster na ndani ya Jengo la Bunge la Uingereza.

Mengi, lakini bado kidogo

Chakula cha mwisho cha usiku alichokula kabla ya kushambulia ilikuwa ni kababu, aliokula katika mgahawa wa bei nafuu katika upande wa kusini wa pwani ya Brighton, kilomita 87 kutoka Uingereza.

Wafanyakazi wa hotelini alikokuwa amelala wamesema hapakuwa na kitu cha kumfanya mtu afikirie kwamba alikuwa katika jioni ambayo ataongeza jina lake katika orodha ya washambuliaji ambao wameuawa wakati wakifanya vitendo vya mauaji huko Ulaya.

Alikuwa mcheshi na mwenye furaha, na aliwaambia wafanyakazi kwamba anawatembelea marafiki Brighton, hoteli iliyoko pembezoni mwa bahari ambako watu wengi huzuru kwa masaa kadhaa na kurejea nyumbani na hivi karibuni eneo hilo lilikuwa linahusishwa na mashoga.

Meneja wa hoteli amewaambia waandishi gaidi huyo alikuwa “akicheka na akifanya mzaha akiwasimulia wapi aliishi” masaa kadhaa kabla hajafanya shambulizi.Lakini tabia yake ya uvunjifu wa amani pia inafahamika—kuanzia vitendo vya ugomvi mpaka kumkata mtu usoni katika ugomvi wa kwenye baa.

Maisha ya utotoni Kent

Idhaa za televisheni za Uingereza Ijumaa zilionyesha picha za Khalid Masood alipokuwa shuleni, wakati huo akijulikana kama Adrian Russel Ajao—jina la familia linalotokana na baba yake wa kambo.

Mtu huyu alizaliwa siku ya Chrismas, 1964. Kama mtoto wa shule katika eneo lenye uchachamavu na kuvutia linalokaliwa na watu weupe zaidi alikuwa mpenzi wa soka, akicheza rugby, na akaingia katika kujenga misuli na pia aliwahi kujaribu madawa.

Rafiki wa utotoni wa mtu huyu ametoa fununu inawezekana akawa alikuwa mlengwa wa aina fulani wa ubaguzi shuleni.

“Alikuwa mwigizaji mkubwa, anapenda marafiki na kucheka,” Kenton Till ameliambia gazeti la Uingereza Daily Mail.

Inawezekana akawa ndio mtoto wa kiafrika pekee katika shule hiyo. Alikuwa amepitia katika aina kidogo ya ubaguzi,” ameongeza kusema, lakini, “sio sana kwa sababu alijaribu kuwa maarufu.”

Till aliendelea kusema kuwa: “Tulikuwa tukishirikiana pamoja mpaka tulipomaliza shule lakini aliwahi kuja kwenye sherehe nyumbani kwangu pamoja na baadhi ya marafiki baada ya kuvuta bangi na mama yangu aliwafukuza wote. Baada ya hapo tukapoteza kwa namna fulani mawasiliano.”

Katika siku za karibuni baada ya kumaliza shule, alikuwa akifanya kazi katika shamba la familia, akiuza bidhaa za kusafishia na akawa anaishi na mwanamke ambae alikuwa mdogo kwake kwa miaka minne.

Lakini baadae kwa sababu ambazo hazikuweza kufahamika kila kitu kikawa kimevurugika.

Polisi mara kwa mara walikuwa wanaitwa nyumbani wake, nyumba aliokuwa akiishi na yule aliyekuwa wakati huo mke wake Jane Harvey, ambae alimzalia watoto wawili kati ya watoto watatu wa Khalid Masood.

Marafiki waliliambia gazeti la Sun Newspaper kuwa Khalid Masood alikuwa akigombana baada ya kunywa. Lakini familia hiyo ikaachana mwaka 2000 baada ya kumkata usoni mmiliki wa baa kesi ambayo ilimfanya Masood afungwe kwa miaka miwili.

Muuaji huyu alilaumu ubaguzi kwa kupigana kwake, akiiambia mahakama alimkata mmiliki wa mgahawa usoni kwa sababu watu wa eneo alilokuwa anaishi katika kijiji cha East Sussex “walimuonyesha chuki” wakati huo alipokuwa anaishi huko.

Jaji aliyemhukumu alitoa angalizo: “Wakati huna fursa ya kutoa kisingizio chochote kwa tabia yako, inaweza kutoa maelezo kwa kiwango fulani .”

Lakini tabia yake ya uvunjifu wa amani katika takriban kesi zote zinazohusu maeneo yote ya umma dhidi yake kwa miaka mingi ziliendana na tabia yake ya ulevi—kabla ya tukio la mwaka 2000 katika ugomvi wa kwenye baa ambapo alikuwa amekunywa pint nne za beer.

Wakati historia ya utotoni na saikolojia ya Khalid Masood inaumuhimu kwa wataalamu wa misimamo mikali (na vyombo vya habari vya Uingereza), ambao wanataka kujua nini kilimpelekea kuuwa, hilo ni jambo dogo kwa wachunguzi wa polisi ambao wana masuali yanayo husu matukio ya sasa na masuali muhimu ambayo yanahitaji majawabu—kati ya hayo, ni lini, kwa nini, na vipi alikuwa ameingizwa katika misimamo mikali.

Wakati polisi wakipekuwa historia ya Maisha yake ya siku za nyuma, wanataka kugundua mara moja kama alifanya hilo shambulio kwa uamuzi binafsi au alikuwa ameelekezwa kuwalenga Bunge la Uingereza. Je alikuwa ni sehemu ya mtandao wa watu wenye misimamo mikali ambao wanaendelea na mipango ya mauaji?

Miaka miwili gerezani

Tarehe za kubadilisha kwake dini kuingia Uislamu hazijulikani, lakini inadhaniwa kuwa aliingia katika siasa kali wakati akitumikia kifungo cha miaka miwili kwa kosa la kumkata mtu na panga mwaka 2000 katika baa.

Katika nchi kadhaa za Ulaya, wengi ambao wanaingizwa katika siasa hizo kali ni wale ambao ni walitenda vitendo vya jinai.

Hakuna maungano ya makundi ya wahalifu na kikundi cha Islamic State na makundi mengine ya wapiganaji lakini yako mafungamano fulani ya makundi ya kijamii, mazingira na vijana. Makundi ya wahalifu na magaidi huwapata wafuasi wao katika makundi hayo, wakitengeneza mahusiano, wanasema wachambuzi.

Watu ambao walifanya mashambulizi Paris 2015 na Brussels walikuwa na historia ndefu ya utukutu utotoni mwao—na baadhi yao wanajulikana kuwa waliingizwa katika makundi hayo wakati wakitumikia kifungo jela, au waliingizwa na watu ambao walikuwa wameambukizwa siasa kali wakati wakiwa jela.

Tangu siku ya Jumatano polisi wamekuwa wakipekua nyumba kadhaa ndani ya Uingereza na wamewakamata watu 11 mpaka sasa, wengine kama ni washukiwa wanaojihusisha na kuandaa vitendo vya ugaidi. Kati ya hao ni mtu mwenye umri wa miaka 27 kutoka Birmingham na mwanamke, miaka 32, kutoka Manchester.

“Wote hawa wanahojiwa wakati tukijaribu kuunga vipande vya taarifa tulizokusanywa katika kile kilichotokea katika shambulio hilo,” afisa wa ngazi ya juu wa polisi ameiambia VOA.

Uchunguzi huo wa polisi, unaoitwa “Operation Classific” unaongozwa na maafisa kutoka SO15, Kikundi cha kupambana na ugaidi cha Polisi, Jijini London.

Kaimu Kamshina Msaidizi Mark Rowley Ijumaa amesema: “Hivi sasa hakuna ushahidi wa tishio lolote zaidi lakini utaelewa kuwa nia yetu ni kujua iwapo alitenda haya peke yake na kushawishiwa na propaganda za magaidi; au, watu wengine wamemsaidia, wamempa moyo na kumuelekeza afanye hivyo.”

Dakika tatu kabla ya kuendesha gari aina ya Hyundai SUV alioikodi na kuwagonga watembea kwa miguu, alioipeleka upande wao wakati wanatembea kuvuka daraja la Westminster Bridge, Khalid Masood alikuwa amefanya mawasiliano na mtu kupitia WhatsApp.

Polisi wanajaribu kumtambu mtu huyo alikuwa ni nani na walikuwa na mazungumzo ya aina gani.

Miaka aliyokuwa Saudi Arabia

Alikokuwa anaishi katika siku za nyuma kumewafanya wachunguzi kutaka kujua zaidi. Kwa mujibu wa maafisa wa polisi wa London walio ongea na VOA, Khalid Masood inasadikiwa aliwahi kuishi kwa miaka kadhaa Saudi Arabia.

Gazeti la The Sun limeripoti kuwa alihamia nchi hiyo mwaka 2005 na kwa miaka minne aliwafundisha kiingereza wafanyakazi wa taasisi ya usafiri wa angani huko Yanbu.

Je, Saudi Arabia ndiko alikobobea katika msimamo mkali?

Mwaka 2009 alihamia Luton, kaskazini mwa London ambako tena alikuwa anafundisha Kiingereza, part-time. Kuchagua kwake kwenda Luton kunaweza kuwa na umuhimu fulani kama ilivyokuwa uamuzi wake wa kuhamia Birmingham. Miji hiyo miwili imeonyesha wazi kuweko kwa kikundi cha kigaidi cha Islamic State chenye kuwaingiza raia wa Uingereza kwenye ugaidi.

Washambuliaji waliotumia mabomu July 7, 2005 London walikuwa na mafungamano na mji huo na miji yote hiyo imekuwa ikitembelewa na wahubiri wenye siasa kali, akiwemo siku za nyuma Abu Hamza, Omar Bakri Mohammed na Anjem Choudary, ambae ni mhubiri maarufu mwenye siasa kali aliyefungwa mwaka jana kwa makosa ya ugaidi na amehusishwa na njama za kupanga vitendo vya ugaidi mara 15 tangu mwaka 2000.

Ilikuwa wakati yuko Luton na Birmingham, ndipo vyombo vya upelelezi vya Uingereza vilipoanza kumfuatilia Khalid Masood.

Alionekana pia na majirani zake huko Luton kama “mkazi,” lakini mmoja wa majirani zake alimuelezea kwa waandishi wa Uingereza alikuwa anaishi kama “kivuli.”

“Sikuwa namuona mara kwa mara. Mara nyingine namuona akitembea usiku. Sikuwa namuona mchana. Ilikuwa tabu kujua anaishi eneo hilo.”

Kwa polisi wa Uingereza, wasiwasi wao ni kuwa inawezekana walipitwa na umuhimu wa kuwatambua “majirani hatari” wengine.

XS
SM
MD
LG