Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limetoa wito kwa Umoja wa Afrika kuanzisha mahakama itakayosikiliza kesi za unyanyasaji mbaya uliofanyiwa watu wa Sudan Kusini, ambako linasema wanajeshi na waasi wametekeleza vitendo vibaya zaidi vya ukiukaji wa haki za binadamu.
Human Rights Watch imesema leo Jumatatu kwamba ina ushahidi wa mauaji, ubakaji na ufurushwaji wa lazima uliotekelezwa na vikosi vya serikali ya Sudan Kusini katika jimbo la Equitoria Magharibi.
Mwezi jana, afisa wa Umoja wa Mataifa, Ivan Simonovic, alilitaja jimbo hilo la Equitoria Magharibi kama sehemu mpya ambako visa vya ukiukaji wa haki za binadamu na uharibifu wa mali uliripotiwa. Shirika hilo limesema watafiti walitembelea eneo hilo mwezi jana na mashahidi walieleza jinsi walivyowaona wanajeshi wakiteketeza majumba, kuiba na kuwafurusha maelfu ya wakaazi kutoka makwao.