Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 16, 2024 Local time: 22:43

UN yataka hatua zaidi katika mapambano dhidi ya Malaria


Wafanyakazi wa huduma Indonesia wakipiga dawa ya kuzuia mbu wa malaria.
Wafanyakazi wa huduma Indonesia wakipiga dawa ya kuzuia mbu wa malaria.

Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Malaria Duniani yanasherehekea maendeleo yaliyopatikana katika kuondoa ugonjwa huo. Shirika la Afya Ulimwenguni linatoa wito kwa hatua kuchukuliwa juu ya mafanikio haya na kuendelea na kazi ya kuunda ulimwengu usio na malaria.

Licha ya janga la COVID-19 na machafuko mengine mengi, nchi 24 zinaripotiwa kusimamisha maambukizi ya malaria kwa miaka mitatu au zaidi hadi mwisho wa mwaka 2020. Kufikia sasa, nchi 38 na maeneo kadhaa yamethibitishwa kuwa hayana malaria na Shirika la Afya Ulimwenguni,-WHO ikiwa ni pamoja na hivi karibuni nchi za El Salvador, Algeria na Sri Lanka.

Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Tedros Adhanom Ghebreyesus, anasema kuondoa malaria ni lengo linalofaa kwa nchi zote, bila kujali inaweza kuwa umbali gani kutoka kwenye lengo kuu.

Malaria ni ugonjwa unaoweza kuzuilika na kutibika. Hata hivyo, kila mwaka unaua zaidi ya watu 400,000, wengi wao wakiwa watoto wadogo barani Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kwa kuongezea, zaidi ya watu milioni 200 huambukizwa ugonjwa huu hatari wa vimelea kila mwaka.

Katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, WHO inaripoti zaidi ya vifo milioni 7.5 na visa bilioni 1.5 vimezuiliwa, hasa katika Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara. Licha ya maendeleo haya ya kushangaza, mkurugenzi wa Mpango wa Malaria wa Ulimwenguni wa WHO, Pedro Alonso, anasema visa na vifo vingi vinaendelea kutokea barani Afrika.

WHO inasema kujitolea kisiasa ni muhimu katika kumaliza malaria. Shirika hilo la afya la Umoja wa Mataifa limesema nchi nyingi ambazo zimeondoa malaria zina mifumo madhubuti ya utunzaji wa afya ambayo inahakikisha upatikanaji wa kinga za malaria, utambuzi na matibabu.

WHO inakadiria hadi dola bilioni 4.5 kwa mwaka itahitajika kumaliza malaria.

XS
SM
MD
LG