Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 10, 2024 Local time: 17:30

Serikali ya Cameroon yatishia kuwakamata viongozi wa upinzani


Rais wa Cameroon Paul Biya alipokutana na rais wa Russia Vladimir Putin wakati wa mkutano wa pili wa Russia na Afrika huko Saint Petersburg Julai 28, 2023. Picha na Artem Geodakyan / AFP.
Rais wa Cameroon Paul Biya alipokutana na rais wa Russia Vladimir Putin wakati wa mkutano wa pili wa Russia na Afrika huko Saint Petersburg Julai 28, 2023. Picha na Artem Geodakyan / AFP.

Serikali ya Cameroon imetishia kuwakamata viongozi wa vyama vya upinzani vinavyotaka kuunda muungano na ushirikiano kwa ajili ya serikali ya mpito ili kumuondoa madarakani Rais Paul Biya, mwenye umri wa miaka 90 ambaye amekuwa madarakani kwa zaidi ya miongo minne.

Waziri wa utawala wa taifa hilo la Afrika Magharibi Paul Atanga Nji, wiki iliyopita aliamuru kukomeshwa kwa shughuli za makundi mawili ya muungano wa kisiasa kwa ajili ya mabadiliko APC na muungano kwa ajili ya mpito wa kisiasa nchini Cameroon ATPC.

Nji amesema vyama vya siasa vilivyo sajiliwa kisheria ndivyo pekee vyenye haki ya kufanya shughuli za kisiasa Cameroon na viongozi na raia wanaojiunga na hayo makundi mawili ya muungno haramu watakamatwa.

Upinzani wa Cameroon na mashirika ya kiraia yanasema marufuku ya shughuli za makundi hayo ni dalili nyingine ya Cameroon kutoheshimu demokrasia na haki za msingi za uhuru wa kujieleza.

Roger Justin Noah ni msemaji wa chama cha upinzani cha Cameroon Renaissance Movement (CRM) kinacho ongozwa na Maurice Kamto, ambaye anadai alishinda uchaguzi wa rais wa Oktoba 2018, na kwamba Rais Paul Biya, alimpokonya ushindi wake.

“Upinzani wa Cameroon hautatishwa na maafisa wa serikali ya Cameroon na wafuasi wa Rais Biya”

“Serikali ya Cameroon imekuwa na hofu kuhusu umaarufu unaokuwa wa kiongozi wa upinzani Maurice Kamto, baada ya mashirika zaidi ya 30 ya kiraia na vyama vya upinzani kujiunga na muungano wa kisiasa wa mabadiliko unaoongozwa na Kamto” alisema Noah.

Vyama vya upinzani vinasema serikali ya Cameroon inaonyesha nia mbaya kwa kupiga marufuku mungano wa upinzani, huku ikiruhusu vyama vingine kukiunga mkono chama tawala cha Rais Biya, cha Cameroon People's Democratic Movement.

Rene Emmanuel Sadi ni waziri wa mawasiliano wa Cameroon na msemaji wa serikali. Anasema hakuna sababu kwa baadhi ya vyama vya upinzani kuunda muungano kwa ajili ya kipindi cha mpito cha kisiasa nchini humo wakati taasisi za serikali zinafanya kazi kikamilifu na rais Biya, anatekeleza majukumu yake kama rais wa Cameroon.

Sadi akiongea na vyombo vya habari wiki hii amesema wapinzani na asasi za kiraia zina wasiwasi juu ya Rais Biya kama atatangaza kuwa mgombea katika uchaguzi wa mwaka 2025.

Forum

XS
SM
MD
LG