Kirill Stremousov, ambaye ni naibu kiongozi wa utawala wa Russia wa sehemu hiyo, ametoa ujumbe wa video kwa wakaazi wa sehemu hiyo baada ya wanajeshi wa Russia kulazimika kurudi nyuma umbali wa kilomita 30 kutokana na mashambulizi ya wanajeshi wa Ukraine.
Wanajeshi wa Ukraine wameimarisha mashambulizi dhidi ya wanajeshi wa Russia ili kudhibithi sehemu ambazo zimechukuliwa na Russia, vita hivyo vikiingia mwezi wa nane.
Wanajeshi wa Ukraine wanalenga kudhibithi sehemu hizo kabla ya kuanza kwa kipindi cha baridi.
Kherson, mji wenye idadi kubwa ya watu, ulichukuliwa na Moscow katika kile imekitaja kama operesheni maalum nchini Ukraine, iliyoanza Februari 24.
Rais wa Russia Vladmir Putin amesema kwamba mji huo sasa ni sehemu rasmi ya Russia, hatua ambayo Ukraine na mataifa ya Magharibi imekataa kutambua.
Mapigano makali yanatarajiwa katika mji wa Kherson
Vita vya Ukraine vimeua maelfu ya watu na kupelekea mamilioni kukosa makazi.
Stremousov amesema kwamba huenda mji wa Kherson ukapigwa makombora na wanajeshi wa Ukraine akiongezea kwamba wakaazi watakaoondoka watapewa makazi nchini Russia.
"Nawaomba mzingatie maneno yangu kwa uzito unaostahili na muondoke haraka iwezekanavyo,” amesema Stremusov, akiongezea kwamba “hatuna mpango wa kuusalimisha mji. Tutaendelea kupigana hadi mwisho.”
Kati ya watu 50,000 na 60,000 wataondolewa mjini humo na kupelekwa Russia katika muda wa siku sita zijazo.
Mji huo ulikuwa na jumla ya watu 280,000 kabla ya vita kuanza, lakini wengi wao wamehama.
"Ukraine inalitayarisha jeshi kubwa sana kwa ajili ya mashambulizi,” amesema Vladimir Saldo akiongezea kwamba "mahali wanajeshi wanafanya shughuli zao, hakuna nafasi kwa raia.”
Russia inatarajia hali ngumu
Hatua ya maafisa wa Russia kuwataka raia kuhama mji wa Kherson, inafuatia tathmini ya kamanda wa jeshi la Russia Jenerali Sergei Surovikin, anayeongoza wanajeshi wa Russia wanaopigana Ukraine kwamba vita vinaendelea kuwa vigumu kwa wanajeshi wa Russia.
"Hali katika sehemu tunayofanya operesheni maalum inaweza kuelezewa kuwa ni ngumu, adui anashambulia miundo mbinu na majengo ya watu kwa makusudi,” Surovikin ameliambia shirika la habari la serikali ya Russia la Russia 24.
Vladimir Rogov, mwanachama wa baraza linalosimamia Zaporizhzhia, sehemu nyingine ambayo Russia ilijinyakulia kimabavu kusini mwa Ukraine, amesema kwamba wanajeshi wa Ukraine wameimarisha mashambulizi ya makombora katika sehemu inayoshikiliwa na wanajeshi wa Russia, ya Enerhodar. Wafanyakazi wengi katika kiwanda cha nyuklia cha Zaporizhzhia wanaishi Enerhodar.