Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 00:38

Russia haitaki uchunguzi wa Umoja wa Mataifa, imepoteza wanajeshi 43, vifaru na silaha


Wanajeshi wakitoa heshima wakati wa mazishi ya kanali Oleksiy Telizhenko, Bucha, Kyiv, Ukraine Okt 18, 2022. Oleksiy alitekwa nyara na wanajeshi wa Russia akiwa nyumbani kwake Bucha. mwili wake ulipatikana umezikwa msituni miezi sita baadaye, karibu na nyumbani kwake.
Wanajeshi wakitoa heshima wakati wa mazishi ya kanali Oleksiy Telizhenko, Bucha, Kyiv, Ukraine Okt 18, 2022. Oleksiy alitekwa nyara na wanajeshi wa Russia akiwa nyumbani kwake Bucha. mwili wake ulipatikana umezikwa msituni miezi sita baadaye, karibu na nyumbani kwake.

Jeshi la Ukraine limeimarisha mashambulizi dhidi ya wanajeshi wa Russia huku serikali ikitangaza mgao wa umeme kote nchini kufuatia uharibifu ambao umetokea kutokana na mashambulizi ya makombora ya Russia ambayo yameharibu mfumo wa umeme.

Katika mji wa Kherson ambao unadhibitiwa na wanajeshi wa Russia tangu walipoingia Ukraine miezi minane iliyopita, uongozi ulioteuliwa na Russia umeanza kuwaondoa watu mjini humo.

Jumatano, naibu wa utawala wa Russia mjini Kherson Kirill Stremousov amesema kwamba Ukraine imeanzisha mashambulizi makali kuelekea Novaya Kamianka na Berislav.

Japo Ukraine haijatoa taarifa yoyote kuhusu operesheni yake, Jeshi lake limesema kwamba wanajeshi 43 wa Russia wameuawa, vifaru sita na silaha nyingine za vita kuharibiwa.

Shirika la habari la serikali ya Russia limeonyesha watu wanaotumia boti wakivuka mto Dnipro wakitoka Kherson. Serikali ya Russia imesema kwamba ni hatua ya kuwaondoa watu kabla ya mapambano makali kuanza.

Karibu watu 60,000 wamepangiwa kuondolewa sehemu hiyo katika muda wa siku sita.

Mgao wa umeme Ukraine

Serikali ya Ukraine imeanza mgao wa umeme, ikiwa ni mara ya kwanza tangu Russia ilipoivamia nchi hiyo. Hatua hiyo imechukuliwa baada ya mashambulizi ya makombora ya Russia kuharibu mfumo wa umeme wa Ukraine.

Shirika la usambazaji umeme la Ukraine, Ukrenergo, limesema kwamba umeme utapatikana kuanzia saa moja asubuhi hadi saa tano usiku.

Russia imeongeza mashambulizi ya makombora dhidi ya mifumo ya nishati na maji ya Ukraine.

Rais wa Ukraine Volodymir Zelenskiy anatarajiwa kuhutubia Umoja wa Ulaya Alhamisi.

Viongozi wa nchi 27 wanachama wa Umoja wa Ulaya watajadiliana kuhusu namna ya kuendelea kuisaidia Ukraine, ikiwemo namna ya kuhakikisha kwamba nchi nzima ina nshati ya kutosha na msaada wa kifedha kwa ajili ya kujenga upya mifumo iliyoharibiwa.

Mashambulizi ya makombora yanaendelea

Mabaki ya ndege isiyokuwa na rubani baada ya kutekeleza shambulizi. Jeshi la Ukraine limesema kwamba ndege hiyo ni ya Iran
Mabaki ya ndege isiyokuwa na rubani baada ya kutekeleza shambulizi. Jeshi la Ukraine limesema kwamba ndege hiyo ni ya Iran

Ndege zisizo na rubani zimeendelea kuushambulia mji wa Mykolaiv kwa makombora.

Ukraine inaishutumu Russia kwa kutumia “Kamikaze” za Iran kutekeleza mashambulizi hayo.

Iran imekanusha ripoti kwamba ndege zake zisizo na rubani zinatumika katika vita vya Ukraine.

Marekani, Uingereza na Ufaransa zimezungumzia ripoti za Russia kutumia ndege za Iran katika vita vya Ukraine, wakati wa kikao cha baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Naibu balozi wa Russia katika Umoja wa Mataifa Dmitry Polyanskiy, amewaambia waandishi wa habari kwamba Russia itathathimini ushirikiano wake na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres na wafanyakazi wake iwapo Guterres atatuma wataalam nchini Ukraine kukagua ndege zisizo na rubani zilizoangushwa, na ambazo Ukraine na mataifa ya Magharibi zinasema kwamba zilitengenezwa Iran.

Wanajeshi wa Russia wanalenga Mashariki mwa Ukraine

Katika sehemu za Mashariki mwa Ukraine, Jeshi la Ukraine limesema kwamba wanajeshi wa Russia wanaendelea kuweka mikakati namna ya kuingia katika miji ya Bakhmut na Avdiivka.

Jeshi la Russia linalenga zaidi kudhibiti mji wa Bakhmut, katika eneo la Donetsk.

Wanajeshi wa Russia wamelenga kuikamata miji 10 katika eneo hilo ikimemo Bakhmut, Soledar na Bilohorivka.

Rais wa Russia Vladimir Putin ameamuru matumizi ya sheria ya kijeshi katika sehemu ambazo Russia ilinyakua kimabavu kutoka kwa Ukraine.

Zelenskiy amewaonya raia wa Ukraine walio katika sehemu ambazo zinadhibitiwa na Russia kukataa jaribio la Russia kuwaingiza katika jeshi, na kuwataka kujaribu kuondoka sehemu hizo.

XS
SM
MD
LG