Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 22:17

Ramaphosa anusurika kura ya kutokuwa na Imani naye bungeni


Rais wa Afrika akusini Cyril Ramaphosa baada ya mkutano na kamati kuu ya chama cha African National Congress (ANC) mjini Johannesburg, Afrika kusini, Dec. 5, 2022.
Rais wa Afrika akusini Cyril Ramaphosa baada ya mkutano na kamati kuu ya chama cha African National Congress (ANC) mjini Johannesburg, Afrika kusini, Dec. 5, 2022.

Rais wa Afrika kusini Cyril Ramaphosa amenusurika kura ya kutokuwa na Imani na utawala wake, baada ya bunge la nchi hiyo kuzima ripoti ya waataalam waliokuwa wakichunguza madai ya utakatishaji wa fedha dhidi yake.

Bunge la Afrika Kusini limetupilia mbali ripoti ya jopo la wataalam wa kisheria ambayo thathmini yake ya awali inasema kwamba huenda Ramaphosa alikiuka maadili kwa kuficha pesa katika shamba lake.

Ramaphosa amekuwa akichunguzwa kutokana na madai kwamba hakuripoti kwa polisi wizi wa kiasi cha dola milioni 4 ulitokea shambani mwake mwaka 2020.

Wizi ulitokea katika shamba la Ramaphosa la Limpopo, kaskazini mashariki mwa Afrika kusini.

Madai hayo yalitolewa na mkuu wa zamani wa idara ya ujasusi.

Ramaphosa amesisitiza kwamba pesa hizo hazikuwa za uma bali zilikuwa zake baada ya kuuza Nyati kwa mfanyabiashara kutoka Sudan.

Wabunge walipiga kura na kupinga ripoti ya uchunguzi. Wabunge wa upinzani walikuwa wamependekeza kwamba kura hiyo ingefanyika kwa njia ya siri, lakini pendekezo lao lilikataliwa.

Wabunge 214 wamepiga kura ya kuzima ripoti hiyo, 148 kuunga mkono na wawili wakasusia upigaji kura.

Wabunge wanne kutoka chama kinachotawala cha African national congress ANC, akiwemo aliyekuwa mke wa rais wa zamani Jacob Zuma Dlamini Zuma, wamepiga kura ya kuunga ripoti ya wataalamu wa sheria, kinyume na matakwa ya kamati kuu ya chama hicho.

Uamuzi wa spika Mapisa

Bunge la Afrika kusini likiwa katika kikao
Bunge la Afrika kusini likiwa katika kikao

Spika wa bunge la Afrika kusini Mapisa Nqakula ametangaza kwamba hakuna mashtaka yanaweza kufunguliwa dhidi ya Ramaphosa, baada ya ripoti ya uchunguzi kuzimwa.

Msemaji wa chama cha ANC Mabe Pule alisema kuwa, msimamo wa kamati kuu ya chama hicho, NEC ni kutupilia mbali ripoti hiyo na kwamba mbunge yeyote atakayepiga kura akiunga mkono ripoti, atakuwa amekiuka maadili ya chama na atashughulikiwa sawa na mtovu wa nidhamu.

Mchambuzi wa siasa za Afrika kusini Peter Bigenda amesema kwamba “ilitarajiwa kuona kwamba rais Cyril Ramaphosa anaondolewa lawama zote na kuwaacha wabunge wa upinzani bila majibu kwa sababu huo ndio utaratibu wa chama cha ANC tangu zamani, kwamba wabunge wote kutoka chama tawala sharti waungane ili kunusuru utawala wa rais aliyeko madarakani kama ilivyotokea kwa Jacob Zuma na Thabo Mbeki.”

Chama cha African national congress kinatarajiwa kuandaa uchaguzi wa kiongozi wake na maafisa wengine wa chama katika kongamano kuu la chama litakalofanyika kuanzia tarehe 16 hadi 20 Desemba mwaka huu 2022.

Kongamano hilo likalofanyika mjini Johannesburg, linatarajia kumpokeza majukumu rais Ramaphosa kuendelea kuongoza ANC, na kugombea hula mwingine madarakani katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2024.

Imetayarishwa na Bryson Bichwa, VOA, Pretoria.

XS
SM
MD
LG